2014-11-30 08:00:24

Kuna maendeleo makubwa katika majadiliano ya kidini na waamini wa dini ya Kiislam!


Baba Mtakatifu Francisko, akiwa mjini Istanbul, Uturuki katika hija yake ya kiekumene, Jumamosi 29 Novemba 2014 alipata nafasi ya kutembelea Msikiti mkuu wa Istanbul unaojulikana kama Msikiti wa Bluu, hapo alipata nafasi ya kusali katika ukimya akiwa ameambatana na Mufti mkuu. Alisikiliza kwa makini sehemu ya Korani Tukufu inayosimulia kutungwa mimba kwa Yohane Mbatizaji kadiri ya mapokeo ya dini ya Kiislam.

Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anafafanua kwamba, hapa Baba Mtakatifu alibaki katika ukimya, huku akiendelea kumwabudu Mwenyezi Mungu katika ukimya wa moyo wake. Wakati wa mazungumzo yake na Mufti mkuu, Baba Mtakatifu Francisko amekazia umuhimu wa waamini kusali na kumwabudu Mwenyezi Mungu, mwingi wa huruma na mapendo, changamoto ya kuendeleza majadiliano ya kidini kati ya Wakristo na Waislam, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya waamini wa dini hizi mbili.

Baba Mtakatifu ametembelea pia Kanisa kuu la Mtakatifu Yustini, moja ya maajabu makubwa ya kiufundi yanayoonesha hekima ya Mungu katika maisha ya mwanadamu, lakini sasa Kanisa hili limegeuzwa kuwa ni Msikiti. Ameangalia kwa umakini mkubwa mahali ambapo viongozi wa Kirumi kutoka Magharibi walikutana na kuzungumza na baadaye akaandika maneno yanayoonesha hekima ya Mungu kwa lugha ya Kigriki.

Baba Mtakatifu amekutana na kusalimiana na baadhi ya waamini waliokuwa wamekusanyika mbele ya Ubalozi wa Vatican nchini Uturuki. Amewashukuru na kuwapongeza wote kwa moyo wa upendo na mshikamano wa dhati katika kukuza na kudumisha majadiliano ya kiekumene yanayojikita katika uhalisia wa maisha yao.







All the contents on this site are copyrighted ©.