2014-11-28 07:47:27

Waamini walei wanatumwa na Mama Kanisa kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji!


Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican kwenye Tamko lao kuhusu Waamini Walei, wanasema, walei wanapaswa kushirikishwa kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa, kwani kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo wanashiriki huduma za Kristo za kikuhani, kinabii na kifalme.

Ushiriki mkamilifu katika maadhimisho ya Sakramenti mbali mbali za Kanisa ni jambo linalohimizwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, sanjari na kukazia maisha ya kiroho, ili kuwawezesha waamini walei kuyatakatifuza malimwengu, wakifanya yote kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu. Waamini walei wajitoe bila ya kujibakiza katika mchakato wa kuinjilisha na kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya ushuhuda amini wa maisha yao, huku wakipenyeza roho ya Kikristo katika medani mbali mbali za maisha.

Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanataka waamini walei kushiriki kikamilifu katika kuanzisha na kuendeleza vyama vya kitume katika ngazi mbali mbali za maisha na utume wa Kanisa mahalia pamoja na kuzingatia mahitaji ya watu sehemu mbali mbali za dunia. Tunu msingi za maisha ya ndoa na familia zipewe kipaumbele cha kwanza; vijana wasaidiwe kukua na kukomaa katika kanuni na misingi bora ya maadili, ili wawe kweli ni "majembe" ya Uinjilishaji miongoni mwa vijana wenzao.

Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA, katika Warsha ya Idara ya Waamini Walei, AMECEA, inasema kwamba, majiundo kwa waamini walei ni kati ya mambo ambayo AMECEA inataka kuyapatia kipaumbele cha kwanza katika shughuli na mikakati yake ya shughuli za kichungaji. Haya yamebainishwa na Askofu Philip Anyoli, alipokuwa anazungumza na wajumbe waliokuwa wanachambua Utume wa Waamini Walei, mkutano ambao umefanyika Jimbo kuu la Dar es Salaam.

Wajumbe wamehamasishwa kuibua mbinu mkakati utakaoimarisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, ili kuweza kukabiliana na changamoto zinazoibuliwa katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Lengo ni kuhakikisha kwamba, Familia inaendelea kuwa ni madhabahu ya Injili ya Uhai; mahali ambapo zawadi ya maisha inapokelewa, inatunzwa na kuendelezwa, hadi kufikia ukamilifu wake. Maisha ya binadamu yanarithishwa kwa njia ya familia, pasi na familia, ulimwengu utatumbukia katika ombwe zito, kwani familia ni msingi wa jamii.

Waamini walei wanakumbushwa kwamba, wao ni sehemu ya majembe yanayotegemewa na Mama Kanisa katika mchakato wa Uinjilishaji mpya, unaozingatia mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili, changamoto ya kuwa kweli ni chumvi na mwanga wa mataifa, kwa kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika medani mbali mbali za maisha, ili kuyatakatifuza malimwengu kama anavyokazia Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI katika Waraka wake wa Kichungaji, Dhamana ya Afrika. Ili kutekeleza dhamana hii, waamini walei hawana budi kulifahamu Neno la Mungu, Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki pamoja na Mafundisho Jamii ya Kanisa, nyenzo muhimu katika kuyatakatifuza malimwengu.

Askofu Telesphori Mkude, Mwenyekiti wa Idara ya Familia, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania amewaambia wajumbe wa Warsha hii kwamba, familia katika ulimwengu mambo leo inakabiliana na matatizo, changamoto na fursa nyingi ambazo Mama Kanisa anapaswa kuziangalia kwa: huruma, uelewa na mapendo, ili kuganga na kuponya madonda yanayoibuliwa ndani ya Familia kwa kutumia huruma na upendo wa Mungu kwa waja wake. Matatizo kama uchumba sugu, ndoa za wake wengi; ndoa za watu wajinsia moja ni changamoto kubwa katika Sakramenti ya ndoa na tunu msingi za maisha ya kifamilia.

Askofu Mkude anasema, maadhimisho ya Sinodi za Maaskofu kwa ajili ya Familia yanayofanyika katika awamu kuu mbili ni jambo ambalo limekuja kwa wakati muafaka, ili kulipatia Kanisa nafasi ya kuangalia changamoto za kichungaji katika maisha ya ndoa na familia, ili kuweza kuwa na mwongozo kamili.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Askofu Desiderius Rwoma, Mwenyekiti wa Idara ya Walei, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, iliyosomwa kwa niaba yake na Askofu msaidizi Methodius Kilaini wa Jimbo Katoliki la Bukoba, ameelezea kwa kina na mapana, matatizo yanayowakumba watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi, kiasi cha kukosa fursa za elimu, afya, malezi na majiundo makini na matokeo yake wanajikuta wakitumbukizwa katika biashara haramu ya binadamu, utumwa mamboleo pamoja na kufanyishwa kazi za suluba, mambo ambao yanahatarisha makuzi, ustawi na maendeleo ya watoto hao.

Askofu Rwoma anasema kwamba, chanzo kikubwa cha ongezeko la watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi ni umaskini, kumong'onyoka kwa: maadili sanjari na misingi bora ya ndoa na familia; sera na mikakati duni ya kijamii na kiuchumi. Umefika wakati kwa Jamii Barani Afrika kusimama kidete kupinga kwa nguvu zote: utumwa wa aina zote wanaofanyiwa watoto, ili kulinda na kudumisha haki zao msingi. Watoto wasifanyishwe kazi za suluba, wala kuhusishwa katika utumwa mamboleo au kupelekwa mstari wa mbele pamoja na kunyanyaswa utu na heshima yao.

Askofu Rwoma amewapongeza Wanawake Wakatoliki wanaoshiriki kikamilifu katika kuyategemeza Makanisa mahalia kwa kuziwezesha Seminari na Nyumba za Malezi kupata mahitaji yao msingi pamoja na kupambana na mila na desturi ambazo zimepitwa na wakati kwa mfano ukeketaji wa wanawake. Kanisa linawashukuru Wanaume Wakatoliki wanaoendelea kulijenga Kanisa kwa juhudi na maarifa pamoja na kutumia vipaji vyao kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo.

Warsha hii imehudhuriwa na wajumbe 60 kutoka katika Nchi za AMECEA na ilikuwa inaongozwa na kauli mbiu "Ndoa na Maisha ya Familia, Kanisa na Jamii kwa siku za usoni. Kwa mara ya kwanza, Warsha hii imehudhuriwa na wajumbe wengi zaidi kutoka katika Nchi za AMECEA, ikilinganishwa na miaka mingine iliyopita. wajumbe kutoka Djibouti, Somalia, Zimbabwe na Mauritius wameshiriki kwa ukamilifu, matendo makuu ya Mungu.

Itakumbukwa kwamba, tangu Mwaka 1975, Baraza la Waamini Walei, katika Nchi za AMECEA lilianzishwa, lakini limeendelea kusinzia kwa miaka yote hii bila hata kutekeleza utume na dhamana yake katika nchi za AMECEA. Mwaka huu, wajumbe wanasema, watajadili hadi kieleweke!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.