Matumaini ya Italia kwa hija ya Baba Mtakatifu nchini Uturuki
Rais Giorgio Napolitano wa Italia anamshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa ujumbe
na matashi mema kwa ajili ya Italia na wananchi wake. Anamtakia kheri na baraka tele
katika hija yake ya kiekumene huko Uturuki, nchi ambayo kwa sasa ina mchango mkubwa
katika kutafuta suluhisho la amani kwa maelfu ya watu wanaoteseka kutokana na vita
inayoendelea huko Mashariki ya Kati, ambayo imepelekea watu wasiokuwa na hatia kupoteza
maisha yao!
Ni matumaini ya Rais Napolitano kwamba, hija hii ya kiekumene itasaidia
kukoleza ari na moyo wa majadiliano kati ya Mashariki na Magharibi; kati ya Waamini
wa dini ya Kiislam na Kikristo; ili kujenga na kudumisha matumaini kwa kesho iliyo
bora zaidi, kwa kutambua tofauti kati ya watu na dini zao, kama utajiri na wala si
kikwazo kati ya watu.