2014-11-24 11:44:11

Utoaji mimba si sehemu ya haki msingi!


Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa linasema kwamba, utoaji mimba si sehemu ya haki msingi za binadamu bali ni kwenda kinyume cha Injili ya uhai, utu na heshima ya binadamu, ni mwelekeo wa jamii kutaka kukumbatia utamaduni wa kifo kwa kisingizio cha uhuru wa wanawake kuamua wanavyotaka kuhusiana na miili yao! Maaskofu wanasema, ni vigumu kuonesha kwamba, utoaji mimba ni sehemu ya haki msingi za binadamu wakati unapelekea mauaji ya kiumbe kisichokuwa na hatia.

Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa linasema kwamba, harakati za kutaka kukuza na kudumisha uhuru na usawa kati ya wanawake na wanaume ni mambo mazuri katika jamii, lakini usawa unaotoa haki ya mtu kushiriki katika mauaji ya watoto wasiokuwa na hatia hapa ni kwenda kinyume kabisa cha haki msingi za binadamu pamoja na kuwasababishia mateso na mahangaiko makuba wanawake wanaoshiriki katika zoezi la utoaji mimba. Kuna kundi kubwa la wanawake linaloendelea kuteseka kisaokolojia na kwa vile waliwahi kushiriki katika zoezi la utoaji mimba, lakini ni mateso na mahangaiko ambayo hayazungumziwi.

Baraza la Maaskofu Katoliki Ufaransa linasema, uhuru ni muhimu sana katika kukuza na kuendeleza mahusiano kati ya mwanaume na mwanamke, wanaotambua dhamana na wajibu wao unaowashirikisha katika kazi ya uumbaji. Kumbe, huu ni uhuru unaowajibisha na kuhamasisha majadiliano ya kina. Kumbe, kuna haja kwa jamii kuangalia kwa makini kwamba, mimba isionekane kuwa ni jambo ambalo halitakiwi na inaweza kuondolewa wakati wowote ule, kwani mtoto aliyeko tumbani mwa mama yake ana haki ya kuzaliwa, kukua na kukomaa kadiri ya mapenzi ya Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.