2014-11-23 08:50:09

Tuzo ya Joseph Ratzinger yatolewa kwa wasomi waliobobea katika Neno la Mungu!


Kardinali Gerhard Ludwig Mùller, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mafundisho tanzu ya Kanisa, kwa niaba ya Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi, tarehe 22 Novemba 2014 alitoa tuzo ya nne ya "Joseph Ratzinger" kwa wasomi waliobobea katika tafiti za kitaalimungu, kama njia ya kuenzi mchango mkubwa uliotolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI katika taalimungu.

Kwa mara ya kwanza, tuzo hii imetolewa kwa Professa Anne Marie Pelletier, Mwanamke, anayefundisha Maandiko Matakatifu katika Chuo Kikuu cha Biblia mjini Paris, Ufaransa, Tuzo hii pia amepewa Padre Waldermar Chrostowski, mtaalamu wa Maandiko Matakatifu anayejibidisha katika kukoleza majadiliano kati ya Wakristo na Wayahudi.

Kardinali Mùller katika hotuba yake amekazia umuhimu kwa Wakleri, Majaalim, Walimu wa dini, wadau mbali mbali katika shughuli za kichungaji na Wakristo katika ujumla wao, kuhakikisha kwamba, wanajibidisha kujisomea na kufanya tafiti kuhusu mchango wa Baba Mtakatifu Benedikto XVI katika taalimungu.

Josefu Ratzinger ni kiongozi kama alivyowahi kusema Papa Francisko aliyefanya tafiti zake za Kitaalimungu kwa kupiga magoti, yaani kazi zake ni matunda ya tafakari ya kina inayosimikwa katika sala. Imani ina nafasi ya pekee katika hija ya maisha ya waamini kwani inawaangazia mwanga katika akili zao ili kutambua mapenzi ya Mungu.

Ikumbukwe kwamba, taalimungu si tu elimu inayomzungumzia Mwenyezi Mungu, bali ni matunda ya ya tafiti makini zilizofanywa na akili mintarafu Neno la Mungu linalozungumza kuhusu Mungu mwenyewe, kwani huu ni mchakato wa majadiliano ya ndani yanayomhusisha binadamu.

Naye Monsinyo Giuseppe Scotti, Rais wa Mfuko wa Joseph Ratzinger, katika hotuba yake ya ufunguzi amewatambulisha washindi wa tuzo hii kuwa ni watu ambao wamefanya hija ya maisha na tafiti zao huku wakiwa wamekamia kusonga mbele kwa imani na matumaini bila ya kuyumbishwa.

Kwa upande wake, Kardinali Camillo Ruini, Rais wa Kamati ya Kisayansi ya Mfuko wa Joseph Ratzinger, amefafanua wasifu na mchango wa Mama Anne- Marie Pelletier na Monsinyo Waldermar Chrostowski. NI watafiti wanaoesha mchango mkubwa wa Kanisa Katoliki nchini Ufaransa katika masuala ya kitaalimungu na uhai katika maisha ya kitamaduni, kama kielelezo makini cha ushuhuda wa Kikristo ndani ya Jamii.

Monsinyo Chrostowski kutoka Poland ni Mhariri mkuu wa Jarida la Kitaalimungu nchini mwake. Ni msomi mwenye ari na moyo mkuu, anayefahamu kwa kina na mapana Maandiko Matakatifu; utajiri anaowashirikisha wengine kwa njia ya kufundisha, tafiti za maisha ya kiroho pamoja na kuwaongoza mahujaji katika maisha yao ya kiroho. Ni kiongozi anayejipambanua kwa kukoleza mchakato wa majadiliano ya kidini kati ya Wakristo na Wayahudi.

Ni mtaalam anayefahamu kuunganisha kanuni za kisayansi na usongo wa Neno la Mungu, kwa ajili ya huduma kwa Kanisa katika mchakato wa maendeleo ya majadiliano ya kidini, changamoto endelevu iliyotoewa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, dhana inayovaliwa njuga kwa wakati huu na Baba Mtakatifu Francisko.







All the contents on this site are copyrighted ©.