Mkicheza na masomo, mtakiona kilichomnyoa Kanga manyoya!
Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Dk. Rehema Nchimbi amewataka wanafunzi wa vyuo vikuu na vyuo
vya elimu ya juu vya mkoa wa Dodoma watumie fursa waliyonayo kuisaidia nchi ya Tanzania
isonge mbele na kufikia uchumi wa juu zaidi. Alitoa nasaha hizo mwishoni mwa wiki
wakati akizungumza na wanavyuo hao kwenye ukumbi wa Chimwaga, Dodoma wakati wa mkesha
wa kusifu na kuabudu (Dodoma Campus Night) ulioandaliwa maalum kwa ajili ya kuwajenga
kimaadili wanafunzi wa vyuo vya mkoa huo.
Dk. Nchimbi ambaye alikuwa Mkuu wa
Mkoa wa Dodoma kabla ya kuhamishiwa Njombe, aliwaasa wanafunzi hao waache kuendekeza
matumizi ya simu za mkononi kwa kutumiana ujumbe ambazo zinawatoa kwenye umakini wa
masomo yao. “Inasikitisha kuona mwanafunzi akiingia mwaka wa kwanza anakuwa mwema,
lakini baada ya muda anarudi nyuma kimaendeleo… kisa meseji anazotumiwa”.
“Muwe
makini na masomo yenu. Angalieni mavazi yenu, angalieni mienendo yenu, jichungeni
msiyumbishwe na tabia za makundi lakini kikubwa zaidi ni kutambua nafasi mlizonazo
na kusimama imara ili kuisadia nchi hii isonge mbele na kufikia uchumi wa juu zaidi,”
alisema.
Mapema, akimkaribisha kuzungumza na wanafunzi hao, Mchungaji Kiongozi
wa Kanisa la TAG-ICC Dodoma, Dk. Gerald Ole Nguyaine aliwaambia wanavyuo kwamba wanapaswa
kuiheshimu nafasi hiyo ya pekee ambayo Mungu amewapa. “Hebu jiulize ni wanafunzi
wangapi ambao wamebaki huko nje na wanatamani kuingia Chuo Kikuu… ni lazima muwe na
dira ili kuitendea haki nafasi mliyoipata. Na kama unataka kuwa mtu ambaye Mungu alikusudia
uwe, ni lazima ujisalimishe kwake,”alisema.
Akitoa mafundisho kwa wanavyuo
hao, Mchungaji Casey Kalaso wa Kanisa la Utume wa Kristo kutoka Kabwe, Zambia aliwataka
wanavyuo hao watambue kuwa mafanikio yanakuja pale mtu anapofanya maandalizi na kutumia
vizuri fursa aliyonayo. “Changamoto kuwa inayotukabili hivi sasa ni kwa mwanadamu
kutojua majira aliyomo… watu wengi hatujui nini tunapaswa kufanya na kwa wakati gani.
Usipokuwa mwangalifu utalia baadaye wakati ulichezea fursa uliyoipata sasa,” alisema.
Akitumia
mfano wa Samson na Delila kutoka kitabu cha Waamuzi (sura ya 13), aliwataka waithamini
nafasi waliyonayo kwani ikipotea ni nadra kuipata tena na kuitumia vizuri. “Usiangalie
mambo ya nyuma, angalia nafasi ya sasa unayopewa na Mungu na uifanyie kazi. Jihadhari
na watu wanaokuja maisha mwako, wako wanaokuja kukuongezea thamani lakini wengine
wanakuja ili kukufanya uwe dhaifu zaidi,” aliwaonya.
Naye Mchungaji Mathew
Sasali wa Kanisa la TAG Mbeya aliwataka wanavyuo hao wajitambue nafsi zao na kubaini
ni picha gani ambazo zimechorwa maishani mwao kama kweli wanataka kusonga mbele maishani
mwao. “Kuna watu waliambiwa hutafaulu kwa sababu katika ukoo wenu hakuna msomi, au
fulani hutaolewa kwa sababu katika familia yenu hakuna aliyewahi kuolewa. Hizo zote
ni picha zinazochorwa kwenye maisha ya watu na kuwazuia kufikia malengo wanayotamani
kuyapata maishani mwao,” alisema.
“Kama hujagundua kuwa kuna picha imechorwa
maishani mwako ni lazima tu itakutesa. Hiyo picha inatabiri ni vita ya aina gani unapigana
nayo. Na usipoifuta hiyo picha, huwezi kutoka kwenye maisha uliyonayo… iwe ni ulevi,
uzinzi, uvivu, na kadhalika,” alisema.
Alisema njia pekee ni kuibadilisha na
kupambana na picha iliyowekwa mbele ya maisha yao. “Picha iliyo mbele yako siyo ile
ambayo Mungu ameileta mbele yako. Taifa la Israel lisingeweza kwenda mbele kama picha
nyingine isingechorwa mbele yao ambayo ilibadilishwa na Yoshua na Kaleb,” alisisitiza.
Ninawasihi
tuchane picha zilizoletwa mbele yetu, iwe na ndugu, marafiki, wanaukoo au wachawi.
Tuchukue hatua na kuikataa picha iliyo mbele yetu ambayo iko nje ya mpango wa Mungu.
Fahamu zetu zikifunguka na kuiona picha ya Mungu, ndipo tutaanza kuchanua na kufanikiwa,”
alisema.
Katika Campus Night hiyo ambayo ilihudhuriwa na wanavyuo zaidi ya
5,000, yalifanyika pia maombi kwa ajili ya vijana wote wa Tanzania, uchaguzi wa Serikali
za Mitaa, Uchaguzi Mkuu wa 2015 pamoja na mchakato wa Katiba Inayopendekezwa. Wanavyuo
hao wa dini mbalimbali wanatoka vyuo vikuu vya Dodoma (UDOM), St. John’s, Vyuo vya
Mipango, Madini, Mirembe, Hombolo, Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) na vyuo vya ualimu
vya Mitumba na Capital.