2014-11-23 14:26:55

Igeni: imani, mapendo na matumaini kutoka kwa Watakatifu wapya!


Sherehe ya Yesu Kristo Mfalme wa ulimwengu ni mwaliko kwa waamini kumwangalia Yesu ambaye ni Mfalme wa kweli na uzima; utakatifu na neema; haki, mapendo na amani. Waamini wanaoneshwa jinsi ambavyo Yesu mwenyewe amemwilisha ufalme huu katika historia na maisha ya mwanadamu kwa kujionesha kuwa ni mchungaji mwema anayepanda na kuwaongoza kondoo wake kwenye malisho ya majani mabichi, anawatafuta wale alipotoea na kuwaganga wagonjwa na wale waliopondeka moyo! Yesu ni kielelezo kwa viongozi wa Kanisa ambao wanahamasishwa kuwa ni wachungaji wema wanaojitofautisha na wevi na wanyang'anyi!

Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Ibada ya Misa katika maadhimisho ya Sherehe ya Kristo Mfalme sanjari na kuwatangaza Wenyeheri sita kuwa ni watakatifu. Yesu kwa njia ya ufufuko wake, ameshinda kifo na mauti na hivyo anatawala milele huku akiwaonjesha watu upendo na wokovu.

Injili inaonesha jinsi ambavyo Yesu atakavyotoa hukumu ya mwisho, kwa kuwashirikisha wateule wake Ufalme wa Mungu ulioandaliwa kwa ajili yao tangu milele, kwani walionesha upendo na mshikamano kwa maskini pamoja na wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa Jamii. Wokovu unapata chimbuko lake pale mwamini anapojitahidi kuiga matendo ya huruma yanayoonesha utimilifu wa Ufalme wa Mungu, kwani matendo haya ni kielelezo cha upendo wa Mungu kwa binadamu. Watu watahukumiwa kwa jinsi ambavyo wamemwilisha upendo huu kwa jirani zao, kwa njia ya ukarimu na mshikamano, kiini cha Injili.

Watakatifu wapya ni kielelezo makini cha watu waliojisadaka kwa ajili ya upendo kwa Mungu na jirani, kila mtu akajitahidi kuchangia kadiri ya uwezo wake katika ujenzi wa Ufalme wa Mungu. Ni watakatifu waliojipambanua kwa huduma makini kwa maskini, wagonjwa, wazee na mahujaji pamoja na kutoa katekesi; wakaonesha mkazo zaidi kwa wale waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa jamii, hawa ndio waliobarikiwa na Mwenyezi Mungu.

Baba Mtakatifu anasema, kwa njia ya kuwatangaza Wenyeheri kuwa watakatifu, Kanisa limekiri Fumbo la Ufalme wa Mungu kwa kumheshimu Kristo Mfalme na Mchungaji mwema, anayeonesha upendo wa hali ya juu kwa Kondoo wake. Watakati wapya wawasaidie na kuwaombea waamini kukua katika furaha ya kutembea katika njia ya Injili na kuimwilisha, ili iweze kuwa ni dira katika maisha. Waamini wajifunze kutoka kwa watakatifu wapya: imani, mapendo na matumaini yasiyofifia kamwe bila kumezwa na malimwengu.

Watakatifu waliotangazwa na Baba Mtakatifu wakati wa Maadhimisho ya Sherehe ya Kristo Mfalme, ambao historia ya maisha na utume wao imesomwa na Kardinali Angelo Amato, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la kuwatangaza waamini kuwa wenyeheri na watakatifu ni hawa wafuatao:

    Giovanni Antonio Farina
    Kuriakose Elias Chavara wa Familia Takatifu
    Ludovico Casoria
    Nicola de Longobardi
    Eufrasia Eluvathingal wa Moyo Mtakatifu wa Yesu
    Amato Ronconi









All the contents on this site are copyrighted ©.