2014-11-22 14:49:21

Pyaisheni karama zenu; wapokeeni na kuwasindika vijana ili kujenga umoja!


Kongamano la tatu la Vyama vya kitume na Jumuiya mpya, lililokuwa linaongozwa na kauli mbiu "Furaha ya Injili: ni furaha ya kimissionari" lililoandaliwa na Baraza la Kipapa la Walei, limejadili kwa kina na mapana changamoto inayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko ya kukuza na kukoleza ari na moyo wa kimissionari ili kuwashirikisha wengine Injili ya Furaha, kwa kutambua kwamba, wanaitwa kutoka katika ubinafsi wao, ili kuanza hija ya maisha ya kiroho kwa ajili ya kuwashirikisha wengine Injili ya Furaha, huku wakiwa wanaongozwa na Roho Mtakatifu.

Itakumbukwa kwamba, kongamano la kwanza lilifanyika kunako mwaka 1998 na kuongozwa na Mtakatifu Yohane Paulo II na Kongamano la pili likaitishwa chini ya uongozi wa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI kunako mwaka 2006. Baba Mtakatifu Francisko akizungumza na wajumbe wa kongamano hili, Jumamosi, tarehe 22 Novemba 2014 amekazia kwa namna ya pekee kabisa wongofu wa ndani na utume wa Kanisa, ni nyenzo muhimu katika mchakato wa kumwilisha imani katika matendo.

Vyama vya kitume na Jumuiya mpya za Kikristo zinaanza kuonesha ukomavu unaopaswa kujikita katika wongofu ili kuendeleza dhamana ya Uinjilishaji pamoja na kuendelea kudumisha karama ya vyama vyao vya kitume; huku wakiwapokea na kuwasindikiza wale wanaotamani kushiriki karama hizi, ili kujenga umoja na mshikamano kwa kuzingatia uhuru wa mtu.

Baba Mtakatifu anasema, vyama vya kitume havina budi kuendeleza karama ambayo vimepokea kutoka kwa Roho Mtakatifu, huku vikionesha ujasiri wa kiinjili mintarafu kweli za Kiinjili na kwamba, vinapaswa daima kurudi kwenye chemchemi ya karama zao, ili kuchota nguvu mpya ya kukabiliana na changamoto mamboleo.

Baba Mtakatifu anakumbusha kwamba, vyama hivi havina budi kuwapokea na kuwasaidia vijana wa kizazi kipya, kwa kutambua kwamba, wao pia ni sehemu ya binadamu ambaye ana madonda makubwa moyoni mwake yanayotokana na matizo katika familia ya binadamu, kiasi cha kukosa utambulisho na kuona ugumu katika kufanya maamuzi magumu katika maisha. Waamini washinde kishawishi cha kuuza uhuru wao kwa watu wengine, hali ambayo itawafanya washindwe kukua na kukomaa.

Majiundo makini ya Kikristo yanapania kumsindikiza mwamini kwa uvumilivu na unyenyekevu mkubwa pamoja na kusoma alama za nyakati kama anavyofanya Yesu mwenyewe. Uvumilivu ni njia pekee kabisa ya kuonesha upendo wa kweli sanjari na kuimarisha mahusiano ya karibu na Kristo, Yesu.

Baba Mtakatifu anasema, umoja ni paji kutoka kwa Roho Mtakatifu na kielelezo cha neema ya hali ya juu ilitolewa na Yesu Kristo kwa njia ya Fumbo la Msalaba, ili watu waweze kutambua kwamba, kweli ametumwa na Baba yake wa mbinguni wakiona wafuasi wake wakiwa wameungana, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa umoja badala ya kuendekeza kinzani na migawanyiko, kwani wote wanafanyika ndugu wamoja kutokana na Damu Azizi ya Yesu iliyomwagika kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu.

Vyama vya kitume na Jumuiya za Kikristo hazina budi kuwa ni sehemu ya Kanisa kwa kuheshimu viongozi halali waliowekwa. Umoja huu ujioneshe kwa namna ya pekee katika kudumisha misingi ya Injili ya Maisha, Familia, Amani sanjari na kusimama kidete kupinga umaskini wa hali na kipato; kwa kukuza uhuru wa kidini na elimu ya dini. Vyama hivi vishikamane kwa ajili ya kuganga na kuponya madonda ya utandawazi yanayomsahau Mwenyezi Mungu na tunu msingi za maisha ya kiroho na kiutu, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa vitu!

Mwishoni, Baba Mtakatifu Francisko anasema, ili kupyaisha karama, kuna haja ya kuheshimu uhuru wa mtu, ili kudumisha umoja na mshikamano; mambo yanayojikita katika wongofu wa kimissionari, nguvu inayoweza kuwasaidia kushinda mapungufu yao ya kibinadamu, tayari kuwatangazia watu Habari Njema ya Wokovu. Toba na wongofu wa ndani ni njia murua kabisa ya kushiriki katika utume wa Kristo, anayewaongoza na kuwasindikiza katika mchakato wa Uinjilishaji.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.