2014-11-21 12:02:49

Msilete makwazo kwa wale wanaotafuta huduma Kanisani!


Katika Siku kuu ya Bikira Maria kutolewa Hekaluni, sanjari na Maadhimisho ya Siku ya Watawa wa Ndani, Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican amewataka wale wote wanaotekeleza utume wao ndani ya Kanisa kuwa makini, ili kamwe wasiwe ni kikwazo kwa watu wanaotafuta huduma, kwa kutambua kwamba, Kanisa au Hekalu ni nyumba ya Sala na Ibada, mahali ambapo Mafumbo matakatifu yanaadhimishwa.

Waamini wengi ni watu wema, lakini wakati mwingine wanakumbana na viongozi ambao wana uchu wa mali na madaraka na matokeo yake wanakuwa ni vikwazo vya maendeleo ya kiroho na kimwili. Baba Mtakatifu anawataka Wakleri kutekeleza wajibu wao kikamilifu na kamwe Kanisa lisigeuzwe kuwa ni soko la biashara, hali ambayo itawafanya Wakleri kumezwa na malimwengu. Sakramenti za Kanisa ni kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya waamini na wala si biashara! Hakuna fedha inayoweza kulipa thamani ya Sakramenti za Kanisa.

Baba Mtakatifu anaonya kwamba, hata kuna baadhi ya wafanyakazi wanaotoa huduma zao ndani ya Kanisa wanaodiriki kuomba rushwa ili kupatiwa huduma, jambo ambalo kimsingi ni kikwazo kwa waamini. Watu wamechoka kusikia na kuona makwazo yakitendwa na viongozi wa Kanisa kutokana na uchu wa fedha. Waamini hawawezi kuwasamehe Wakleri wanaojishikamanisha sana na fedha au wale wanaowanyanyasa waamini wao. Hakuna mtu anayeweza kuwahudumia Mabwana wawili: Kanisa na Fedha!

Baba Mtakatifu anasema, Yesu amekuja kumkirimia mwanadamu ukombozi kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wake na wala kwa fedha, ili kuwaonjesha watu huruma na upendo wa Mungu. Kanisa linapokumbatia fedha, hapo linakwenda kinyume kabisa na utashi wa Yesu mwenyewe, ndiyo maana Yesu alitembeza mkng'oto Hekaluni, ili kuwafukuza wale waliokuwa wamegeuza Hekalu kuwa ni pango la wevi na wanyang'anyi. Siku kuu ya Kutolewa kwa Bikira Maria Hekaluni, ni mwaliko kwa wote wanaohusika kuhakikisha kwamba, wanaendelea kulitakatifuza Kanisa, ili kuwaonjesha huruma na upendo, wale wote wanaokuja kutafuta huduma kana kwamba ni Bikira Maria.







All the contents on this site are copyrighted ©.