2014-11-19 14:11:45

Kila mwamini anaitwa kuwa Mtakatifu!


Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Katekesi yake, Jumatano, 19 Novemba 2014 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican ameendelea kutafakari kuhusu Kanisa, lakini kwa kukazia wito wa utakatifu unaotolewa kwa waamini wote, kutokana na dhamana ya Ubatizo, kila mwamini anatakiwa kuwa Mtakatifu.

Baba Mtakatifu anakumbusha kwamba, utakatifu kwanza kabisa ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu na wala si matunda ya juhudi za mtu binafsi. Mtakatifu Paulo anakumbusha kwamba, Yesu alilipenda Kanisa kiasi cha kujisadaka, ili liweze kuwa takatifu. Kwa njia ya umoja na Kanisa, kila Mkristo ametakatifuzwa kwa neema ya Sakramenti ya Ubatizo na hivyo anatakiwa kukua na kukomaa katika utakatifu.

Waamini wanaalikwa kumwilisha hafuru ya utakatifu katika medani mbali mbali za maisha yao ya kila siku, wanapotekeleza dhamana na majukumu, daima wajiweke katika hali ya sala, huku wakiwa wameungana na Mwenyezi Mungu pamoja na jirani zao. Baba Mtakatifu anawauliza waamini na wote wenye mapenzi mema ni kwa kiasi gani wamejizatiti katika kuchuchumilia wito wa utakatifu wa maisha? Ili kuishi katika utakatifu, Yesu anawaalika wafuasi wake kuonja furaha inayobubujika kutoka kwake, ili waweze kuwaonjesha wengine mapendo.

Mtu anapokua na kukomaa katika utakatifu, ina maana kwamba, anakuwa ni mtu mwema zaidi, asiyezongwazongwa na ubinafsi na hali ya kujitafuta mwenyewe na daima yuko tayari kujisadaka kwa ajili ya huduma kwa wengine kama wakili mwema wa neema mbali mbali za Mungu. Amewataka waamini kujenga na kuimarisha upendo na mshikamano kati yao, kwa kutambua kwamba, Yesu daima anaendelea kuambatana nao katika hija ya maisha yao ya kiroho, ili siku moja waweze kuwa watakatifu, huku wakiendelea kuonesha uaminifu wao kwa Kristo na Kanisa lake.

Baba Mtakatifu Francisko ametambua uwepo wa wajumbe wanaoshiriki katika Jukwaa la Uchumi Duniani, linaloendeshwa na Vyuo vikuu vya Kipapa mjini Roma, ili kuisaidia Jamii kuondoka na mambo ambayo yanawatenga wengine katika mchakato wa kiuchumi, kwa kutumia nguvu ya fedha, ambayo kwa baadhi ya watu imekuwa kama miungu wadogo. Fedha anasema Baba Mtakatifu inapaswa kutumika kwa ajili ya mafao ya wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.