2014-11-18 09:52:17

Rais wa Serikali ya mpito Burkina Faso apatikana!


Bwana Michael Kafando ameteuliwa kuwa ni Rais wa Burkina Faso katika kipindi cha mpito kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika nchini humo Mwezi Novemba 2015. Bwana Kafando ni mwanadiplomasia mkongwe aliyewahi kuwa Waziri wa mambo ya nchi za nje na Mwakilishi wa kudumu wa Burkina Faso kwenye Umoja wa Mataifa.

Muafaka huu kati ya Jeshi, Wanasiasa na Viongozi wa kidini umefikiwa rasmi hapo tarehe 16 Novemba 2014 baada ya wadau mbali mbali kuweka sahihi ya makubaliano yaliyotoa mwanya kwa Bwana Michael Kafando kuteuliwa ili kuongoza nchi, baada ya kuwapepeta viongozi wengine waliokuwa wamependekezwa katika kinyang'anyiro cha urais nchini Burkina Faso.

Kazi kubwa inayomngoja Rais Kafando kwa sasa ni kuteuwa mtu atakayekuwa Waziri mkuu wa kipindi cha mpito atakayepewa dhamana ya kuteuwa Mawaziri ishirini na watano watakaounda Serikali ya mpito. Bunge jipya litaundwa na wabunge tisini watakaochaguliwa kutoka katika makundi mbali mbali nchini Burkina Faso.







All the contents on this site are copyrighted ©.