2014-11-17 09:39:57

Wahamiaji ni rasilimali na wala si kero wala majanga tu!


Kongamano la Saba la Kimataifa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wahamiaji linaloongozwa na kauli mbiu “ushirikiano na maendeleo katika shughuli za kichungaji miongoni mwa wahamiaji”, linalowashirikisha mabingwa na wataalam 300 kutoka katika nchi 93, kuanzia tarehe 17 hadi tarehe 21 Novemba 2014 linafanyika kwenye Chuo Kikuu cha Kipapa cha Urbaniana, kilichoko mjini Roma.

Kilele cha kongamano hili ni hapo tarehe 21 Novemba, 2014 wajumbe watakapopata nafasi ya kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko mjini Vatican.

Kardinali Antonio Maria Vegliò, Rais wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum katika mahojiano na Radio Vatican anabainisha kwamba, uhamiaji ni tatizo nyeti, kwani wahamiaji ni watu ambao wamebeba ndani mwao: karama, matumaini na matatizo na changamoto za maisha.

Ikiwa kama wahamiaji watatambuliwa na kuthaminiwa wanaweza kuwa ni kichocheo kikuu cha ugunduzi na maendeleo endelevu kati ya watu na kamwe wasichukuliwe kuwa ni kero na mzigo katika jamii wahisani. Hawa ni nguvu kazi ambayo ikitumiwa barabara inaweza kusaidia katika mchakato wa uzalishaji, ni chem chemi ya ushirikiano na umoja kati ya tamaduni, Kanisa na Serikali husika.

Ni watu wanaopaswa kufunda barabara, kupewa fursa za ajira na kushirikishwa kikamilifu katika jamii inayowahifadhi, hapo watakuwa ni watu wenye mafao kwa jamii hisani na kule walikotoka.

Kardinali Veglio’ anakiri kwamba, kati ya changamoto kubwa inayoikabili Jumuiya ya Kimataifa ni kusimamia na kuratibu shughuli za wahamiaji na wakimbizi. Wahamiaji wanakabiliana na changamoto mbali mbali katika medani za kiuchumi, kijamii, kitamaduni na kidini. Wahamiaji wasipodhibitiwa vyema, wanaweza kuwa ni chanzo kikuu cha uhalifu na uvunjaji wa sheria na kanuni za maisha ya watu, hali ambayo wakati mwingine imekuwa ni chanzo cha woga usiokuwa na mashiko wala ustaarabu.

Wahamiaji wamekuwa ni chanzo kikuu cha ukuzaji wa uchumi kwa nchi hisani na kule wanakotoka kwani wanapopata ajira, sehemu ya mapato yao, inarudishwa nchini mwao kwa ajili ya kusaidia maboresho ya maisha ya familia na jamii kwa ujumla. Ni kundi kubwa linalochangia pia ustawi na maendeleo ya Kanisa zima.

Kardinali Veglio’ anasema kwamba, “familia ya wahamiaji” ni kati ya mada nyeti zinazojadiliwa katika kongamano la saba la wahamiaji kimataifa. Hii inatokana na ukweli kwamba, Mama Kanisa anaendelea kuwekeza zaidi katika familia, ili kuiwezesha familia kutangaza Injili ya Familia na matumaini kwa wale waliokata tamaa. Itakumbukwa kwamba, familia ni chemchemi ya maisha, tamaduni, tunu msingi za maisha ya kiutu na kiimani. Ni mwaliko wa kuhakikisha kwamba, Kanisa linasaidia kuganga na kuponya madonda ya familia za wahamiaji, ili ziweze kutekeleza dhamana na utume wake katika jamii husika, kwa kushirikiana na nchi wanakotoka wahamiaji hawa.

Katika mkutano huu, wajumbe pia wanajadili kwa kina na mapana kuhusu dhamana na wajibu wa wanawake katika suala zima la uhamiaji kwa kutambua kwamba, wahamiaji wanawake wanaunda takribani asilimia 49% ya wahamiaji wote duniani. Ni kundi linalotafuta ustawi na maendeleo ya watu wake. Wanawake wakithaminiwa wanaweza kuwa ni vichocheo vya ushirikiano na maendeleo ndani ya jamii.

Kanisa linatambua matatizo na changamoto wanazokabiliana nazo wanawake wanaolazimika kuzihama nchi zao kwa kuacha familia na wakati mwingine wanajikuta wakitumbukizwa kwenye biashara haram ya binadamu na utumwa mamboleo. Vijaana wanaohama kutoka katika nchi zao wakitafuta maisha bora zaidi wanaendelea kuongezeka maradufu, huku wakiwa wamebeba ndani mwao karama na vipaji mbali mbali tayari kushiriki katika mchakato wa maboresho ya kijamii.

Vijana wanapaswa kulindwa na kutunzwa, ili waweze kushirikisha ndoto na mang’amuzi yao ya maisha, kwa ajili ya ustawi na mafao ya wengi. Kanisa limeendelea kuwa mstari wa mbele kuwalinda na kuwatetea vijana wahamiaji katika shida na mahangaiko yao, ili waweze kuwa imara katika utambulisho na imani yao.

Kardinali Veglio’ anasema kwamba, changamoto kubwa kwa sasa ni kuhakikisha kwamba, utu na heshima ya wahamiaji na wakimbizi inalindwa na kutetewa na wengi. Kanisa linapania pamoja na mambo mengine, kuwajengea uwezo waamini ili waweze kusimama kidete kuwalinda na kuwatetea wakimbizi na wahamiaji. Wawasaidie wakimbizi na wahamiaji katika maboresho ya maisha mapya wanapokuwa ugenini, hasa zaidi wanapokumbana na matatizo pamoja na changamoto za maisha.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.