Yaliyojiri huko Assis wakati wa mkutano mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia
Baraza la Maaskofu Katoliki Italia, CEI, hivi karibuni limehitimisha mkutano wake
wa 67 uliokuwa unafanyika mjini Assisi, kwa kuwashukuru na kuwapongeza Mapadre wanaoendelea
kujisadaka kwa hali na mali kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Familia ya Mungu nchini
Italia.
Katika mkutano wao, Maaskofu wamechambua na kukazia umuhimu wa Kanisa
kuendelea kutangaza Injili ya Uhai dhidi ya utamaduni wa kifo sanjari na kujikita
katika majiundo makini kwa Mapadre, ili waweze kutekeleza dhamana na utume wao kwa
ari na moyo mkuu zaidi, wakitambua kwamba, kwa sasa wanahamishwa na Mama Kanisa kuwa
na mwelekeo mpana zaidi wa maisha ya kimissionari, ili kutoka kifua mbele, tayari
kuwatangazia Watu wa Mataifa, Habari Njema ya Wokovu.
Baraza la Maaskofu Katoliki
Italia limepembua tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, matatizo, changamoto na
fursa zilizopo, ili kuliwezesha Kanisa kuendelea kutangaza Injili ya Familia. Wameonesha
mshikamano wa udugu na upendo kwa Wakristo wanaoteswa na kunyanyaswa huko Mashariki
ya Kati, kiasi kwamba, wanalazimika kuzikimbia nchi zao ili kusalimisha maisha yao.
Mshikamano huu, umeoneshwa na Baraza la Maaskofu kwa kundi la Maaskofu kutembelea
huko Nchi Takatifu ili kujionea wenyewe hali halisi.
Baraza la Maaskofu Katoliki
Italia, pamoja na mambo mengine limejadili kuhusu Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani,
utakaozinduliwa hapo tarehe 30 Novemba, 2014 Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio
na kufungwa rasmi tarehe 2 Februari, 2016 Siku kuu ya Kutolewa Bwana Hekaluni, sanjari
na Maadhimisho ya Siku ya Watawa Duniani.
Maaskofu wamefafanuliwa kuhusu maandalizi
ya maadhimisho ya Kongamano la tano la Kikanisa Kitaifa litakalofanyika Jimboni Firenze
kuanzia tarehe 9 hadi tarehe 13 Novemba 2015.
Maaskofu wamehabarishwa kuhusu
maandalizi ya Onesho la Sanda Takatifu litakalofanyika Jimbo kuu la Torino kuanzia
tarehe 19 Aprili hadi tarehe 24 Juni 2015. Maaskofu pia wameanza maandalizi kwa ajili
ya kushiriki katika maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani, itakayoadhimishwa kuanzia
tarehe 26 hadi 31 Julai 2016, Jimbo kuu la Crakovia, Poland.Mwishoni, Baraza la Maaskofu
Katoliki Italia limewaandikia Mapadre barua ya kuwashukuru, kuwapongeza na kuwahimiza
katika maisha na utume wao wa Kipadre kwa ajili ya ustawi wa Kanisa la Kristo na maendeleo
ya watu!