2014-11-14 10:58:23

Wananchi Barani Afrika wanapaswa kujifunga kibwebwe kwa ajili ya maendeleo yao!


Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani amewataka wananchi Barani Afrika kujifunga kibwebwe ili kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika mchakato wa maboresho ya maisha ya watu wa Bara la Afrika, vinginevyo, Jumuiya ya Kimataifa itakuwa inabuni na kupanga mikakati ambayo haiwezi kuzaa matunda yanayokusudiwa. Umefika wakati kwa Bara la Afrika kuwa na mwono mpana zaidi kuhusu mikakati inayoweza kuleta mabadiliko ya kweli kwa wananchi wa Bara la Afrika.

Kardinali Turkson ameyasema haya hivi karibuni alipokuwa anazungumza na wajumbe waliokuwa wanashiriki katika semina ya siku tatu iliyoandaliwa na Chuo Kikuu cha Tangaza, kilichoko, Nairobi, Kenya, iliyokuwa inapania pamoja na mambo mengine kuangalia mbinu mkakati na miundo inayoweza kuleta mabadiliko Barani Afrika kwa kuvishirikisha vyama vya kitume katika mchakato wa maendeleo endelevu.

Kardinali Turkson amesema, NEPAD ilikuwa na mwono na mipango kamambe kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Bara la Afrika, lakini kwa bahati mbaya NEPAD haikujiamini wala kuonesha utashi wa kutekeleza mwono huu katika uhalisia wa maisha ya wananchi wa Bara la Afrika. Umoja wa Afrika kwa sasa unajitahidi kuokota makapi ya mipango na mikakati iliyoshindwa kutekelezwa na NEPAD kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Bara la Afrika.

Vyama vya kitume vinaweza kusaidia kuchochea maendeleo ya wananchi wa Bara la Afrika, lakini ifahamike kwamba, hili ni jukumu la kwanza kabisa ambalo linapaswa kutekelezwa na viongozi wa Serikali na wanasiasa. Kuna ndoto nyingi ambazo zinajikita katika mchakato wa mabadiliko ya kijamii Barani Afrika, lakini ndoto bila kutekelezwa zinabaki kuwa ni ndoto tu! Huu ni mchakato ambao wananchi wa Afrika hawana budi kushiriki kikamilifu, vinginevyo, mipango ya maendeleo itaendelea kubaki kwenye makaratasi.

Naye Askofu mkuu Zacchaeus Okoth, Mwenyekiti wa Tume ya haki na amani Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya amekiri mchango wa Kanisa katika mchakato wa kuandika Katiba mpya kunako mwaka 2010, ili kukoleza maendeleo ya watu nchini Kenya. Lengo ni kumwendeleza mtu mzima: kiroho na kimwili, kwa kulinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu, aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Vyama vya kitume na Taasisi mbali nchini Kenya vilichangia katika kukuza na kuimarisha ukweli na uwazi.







All the contents on this site are copyrighted ©.