Zingatieni: udugu, sala na utume katika majiundo yenu ya Kipadre!
Udugu, maisha ya sala, utume na maisha ya Kanisa ni mambo msingi kwa Majandokasisi
wanaojiandaa kwa ajili ya maisha ya Kipadre ndani ya Kanisa. Ni wosia uliotolewa na
Baba Mtakatifu Francisko kwa Majandokasisi kutoka Ufaransa waliokuwa wanafanya hija
ya maisha ya kiroho kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Lourdes, Ufaransa kuanzaia
tarehe 8 hadi 10 Novemba 2014. Hii ni hija ambayo imewashirikisha Majandokasisi 750
wanaoendelea kufundwa kwa ajili ya maisha ya Kipadre nchini Ufaransa.
Baba
Mtakatifu anawataka Majandokasisi kujenga na kudumisha umoja na mshikamano katika
maisha na utume wao, wakijitahidi kumwilisha Ujumbe wa Injili katika uhalisia wa maisha,
kama kielelezo cha ushuhuda wa utume wao kwa Kristo na Kanisa lake, kwa kuweka kando
ubinafsi. Seminari pawe ni mahali pa kuishi kwa umoja, upendo na mshikamano; mahali
pa kufahamiana na kusaidiana kwa hali na mali pamoja na kuonesha ushuhuda wa pamoja
wa neema inayobubujika kutoka kwa wafuasi wa Kristo wanaojisadaka kwa ajili ya Mungu
na jirani.
Baba Mtakatifu Francisko anawataka Majandokasisi kukua na kukomaa
katika upendo na mshikamano wa kidugu pamoja na kuendelea kumtumainia Roho Mtakatifu,
ili hatimaye, watakapofikia Daraja Takatifu la Upadre, Udugu liwe ni neno ambalo ni
sehemu ya vinasaba vya maisha yao ya kila siku. Majandokasisi wawe ni watu wa sala
na tafakari ya kina kama walivyofanya Mitume pamoja na Bikira Maria walipokuwa wamekutanika
kwenye Chumba cha juu, huku wakisubiri zawadi ya Roho Mtakatifu.
Neno la Mungu
liwe ni taa na mwanga katika maisha yao na kwamba, Sala daima inapaswa kumwilishwa
katika uhalisia wa maisha. Majandokasisi wajitahidi kutumia vyema muda wao kwa ajili
ya Sala, tafakari na Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu, ili kweli Yesu mwenyewe aweze
kuzima kiu ya maisha yao ya ndani. Majandokasisi wajifunze kusali kwa unyenyekevu,
ili kumwachia nafasi Mwenyezi Mungu aweze kuwafunda kadiri ya mapenzi yake na kuwa
kweli ni "Watu wa Mungu".
Baba Mtakatifu anawakumbusha Majandokasisi wanaojiandaa
kwa ajili ya kupokea Daraja takatifu la Upadre kwamba, kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo,
wanashiriki dhamana ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu. Watakapopewa Daraja Takatifu,
watakabidhiwa na Maaskofu wao dhamana kubwa zaidi ya kushiriki katika maisha na utume
wa Kanisa, kwa kuwagawia watu Mafumbo ya Kanisa.
Hapa watakuwa wanatekeleza
amri ya Kristo ya kwenda ulimwenguni kote ili kuwafanya wote kuwa ni wafuasi wake,
huku wakiwabatiza katika Fumbo la Utatu Mtakatifu. Hapa Majandokasisi wanapaswa kujikita
katika fadhila ya unyenyekevu wenye mvuto na mguso katika maisha na utume wa Kimissionari.
Baba
Mtakatifu kwa namna ya pekee, anawasihi vijana kujitahidi kuufahamu ulimwengu, mahali
watakapokutana na watu, wajitahidi kuwatakatifuza kwa njia ya mifano bora ya maisha
yao, hasa kwa kuwaendea wale ambao kwa muda mrefu wamesahau mahali ambapo kuna mlango
wa Kanisa. Wajitahidi kuwaendelea watu wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii bila
ya kuwasahau wale ambao wako mijini, kwa kutambua kwamba, utume wa Kanisa unafumbatwa
katika maisha ya sala, ili kuwa kweli ni wahudumu waaminifu wa Mafumbo ya Kanisa kwa
Familia ya Mungu.
Baba Mtakatifu anawakumbusha Majandokasisi kwamba, Bikira
Maria, Mama wa Mungu na Kanisa katika hija ya maisha yake hapa duniani alijitahidi
kumsindikiza Mwanaye wa pekee katika hatua mbali mbali za maisha na utume wake, hadi
aliposimama pale chini ya Msalaba na kupokea maiti ya Mwanaye! Bikira Maria awasindikize
Majandokasisi katika maisha na majiundo yao, ili kweli waweze kuwa ni wachungaji wema
na watakatifu kadiri ya mpango wa Mungu.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.