2014-11-11 09:46:06

Serikali ya Kenya kuunda timu kuchunguza madai kuhusu chanjo!


Wizara ya Afya nchini Kenya imeunda timu maalum itakayochunguza madai ya Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya kwamba, chanjo ya Pepopunda inayotolewa kwa sasa inataka kudhibiti ongezeko la idadi ya watu nchini Kenya.

Timu ya uchunguzi inatarajiwa kuundwa wakati wowote kuanzia sasa kutona na taarifa iliyotolewa na Bwana James Macharia, Katibu mkuu wa Wizara ya Afya nchini Kenya. Wawakilishi kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya na Chama cha Madaktari Wakatoliki watashirikishwa katika timu hii ya uchunguzi, ili kuweza kujiridhisha kwamba, chanjo inayotolewa kwa wananchi wa Kenya haina madhara yoyote kwa maisha ya watu.

Serikali ya Kenya inasema kwamba, chanjo inayotolewa haina madhara na badala yake, kuna makosa ya kutafsiri chanjo hii yanayofanywa na Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya katika maabara zake. Uchunguzi utafanyika kwa kuzingatia sayansi kwa kuwashirikisha wadau mbali mbali ili kupata ukweli wa mambo kuhusu chanjo hii.

Maaskofu kwa upande wao wanasema, chanjo hii imechafuliwa na homoni ijulikanayo kama "Beta-HCG" ambayo inaweza kusababisha utasa na uharibifu mkubwa wa mimba. Chama cha Walimu wa shule za Msingi Kenya wameungana na Baraza la Maaskofu Katoliki ili kuonesha wasi wasi wao kuhusu chanjo inayotolewa kwa wananchi wa Kenya, kwa hofu kwamba, kama kweli ina madhara, basi, walimu wengi watakosa fursa za ajira kwa siku za usoni, kwani hakutakuwepo na watoto wa kufundishwa tena!







All the contents on this site are copyrighted ©.