2014-11-11 15:37:17

Ni lazima kukataa vishawishi vinavyotuzuia kuhudumia wengine.


Ni lazima kuvishinda vishawishi na vikwazo vinavyo sababisha tushindwe au kujitenga katika kuhudumia wengine. Badala yake, tuzingatie mafundisho ya Yesu, kwamba, ni lazima tuhudumie kwa moyo safi bila kuweka maslahi mbele, na tuepuke kuifanya huduma kuwa nguvu ya kujipatia ufahari au mamlaka. Haya ni maoni ya Papa Francisco, katika tafakari yake wakati wa Misa asubuhi Jumanne hii, akiwa katika kanisa dogo la Mtakatifu Marta, hapa Vatican.

Homilia ya Papa, ililenga katika somo la Injili ya Luka, ambamo mna mfano wa Mtumishi mtumishi asiye na faida. Papa anasema kwamba mfano huu unatufundisha sisi kama Wakristo, nini maana ya huduma. Yesu anazungumzia mtumishi ambaye, baada ya kufanya kazi siku nzima, anarejea nyumbani, na badala ya kupumzika bado anaendelea kumhudumia bwana wake.

Papa alizungumzia hali halisi ya kibinadamu kwamba wengi wangemshauri mtumishi huyo kwenda kutoa malalamiko kwa chama cha wafanyakazi, na kupata ushauri wa jinsi ya kukabiliana na bwana wake. Lakini kumbe katika mtazamo wa Yesu, huduma haina mwisho, kwa sababu huduma ni njia na tabia ya maisha bora. Yesu alisema mwenyewe,amekuja kutumikia na si kutumikiwa. Yeye ni mtumishi wa wote. Anajitoa mwenyewe kama mtumishi, hivyoni wazi , Bwana anaonyesha njia kwa wafuasi wake, na wale wote ambao wamepokea imani kwa ubatizo, kwamba imani ni kuhudumia kwa upendo bila kutarajia malipo. Imani kwa Kristo ni kutembea katika njia yake ya maajabu na huduma.

Papa aliongeza, Mkristo ambaye hupokea zawadi hii ya imani katika ubatizo, lakini ambaye haipeleki zawadi hii kwa wengine kupitia njia ya huduma, anakuwa Mkristo asiyekuwa na nguvu, Mkristo asiyezaa matunda. Na mwisho wake, alionya anakuwa ni Mkristo aliyejifungia yeye mwenyewe, akijihudumia yeye mwenyewe binafsi. Maisha ya namna hiyo, ameonya Papa ni maisha yasiyokuwa na furaha , na hupoteza bure mambo mengi mazuri na wema wa Kristo.

Papa alitaja "Uvivu hutuweka mbali na kazi na huduma, ukiongoza katika maisha ya ubinafsi. Wakristo wengi huanguka katika dhambi hii ya uvivu , wengi wao ni wazuri wenye kushiriki vyema katika ibada za Misa lakini panapokuwa na haja ya kutoa huduma kwa wengine ,hasa kulipeleka neno la mungu kwa wengine, hujitenga mbali,kwa sababu mbalimbali binafsi.

Papa aliendelea kufafanua nini maana ya huduma, kwamba kwake yeye ina maana ya kila jambo, huduma kwa Mungu,ni katika ibada, katika sala, katika kumsifu Mungu na huduma kwa wengine, ni huduma isiyokuwa na mwisho, kwa sababu Yesu yuna nguvu katika hili,na hivyo daima huandamana nao wote walio katika kuhudumia. Na wakati wa kukamilisha kazi , ametuamuru kusema, sisi ni watumishi wasiokuwa na faida. Watumishi wasiotafuta malipo kwa huduma.









All the contents on this site are copyrighted ©.