2014-11-11 14:44:40

FemAct, walaani vurugu dhidi ya Jaji mstaafu Sinde Warioba!


Sisi Mashirika yapatayo 50 yanayotetea Usawa wa Kijinsia, Haki za Binadamu, Demokrasia, Utawala bora, Maendeleo na Ukombozi wa Mwanamke Kimapinduzi (FemAct) tumekuwa tukifuatilia kwa karibu mchakato wa katiba unavyokwenda tangu ulipoanza. Pamoja na changamoto nyingi zilizojitokeza, bado kuna fursa ambazo wananchi wameweza kushirikishwa na kuleta matumaini ya kupata katiba mpya.

Hata hivyo, jambo la kusikitisha ni kwamba wakati mchakato ukikaribia kufikia mwisho , kumeanza kujitokeza matukio ya aibu na ya kusikitisha ambayo yanaweza kuchafua kabisa au kuharibu kazi nzuri ambayo ilikuwa imeanza kufanyika. FemAct imesikitishwa na vurugu za hivi karibuni zilizosababisha kukatishwa kwa mdahalo wa kujadili mchakato wa katiba mpya ya Tanzania huku baadhi ya watu wakipigwa na kujeruhiwa. Watu hao ni pamoja na mwandishi wa habari wa BBC aliyeumizwa, mwanamke moja aliyepigwa na kuangushwa pamoja na kuzingirwa kwa mlemavu wa macho aliyekuwa akishiriki katika mjadala huo.

Mdahalo huo uliokuwa ukirushwa mojakwamoja na redio na televisheni ulivurugika kutokana na kundi la vijana kuanza kumzomea aliyekuwa mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, alipokuwa akiwasilisha hoja zake. Zomeazomea hiyo ilifuatiwa na vurugu ambazo zilisababisha mtafaruku na bugdha kubwa kwa washiriki wa mjadala huo.

Hali hii ni tishio kwa uhuru na haki kwa wananchi kujieleza, kutoa maoni na kujumuika katika kujadili masuala muhimu yanayohusu mustakabali wa nchi yao. FemAct ikiwa ni muungano wa mashirika na asasi mbalimbali za kiraia, inalaani vikali vurugu hizo kwani zinaweza kusababisha machafuko nchini hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa na mchakato wa kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa.

Vurugu kama hizo zina ashiria tishio kwa wananchi hasa makundi yaliyoko pembezoni, wakiwemo wanawake, wazee, walemavu , wagonjwa , watoto , na makundi mengineyo. Ni dhahiri kuwa, makundi hayo na Watanzania kwa ujumla watagubikwa na hofu ya kushiriki katika kujadili katiba inayopendekezwa ambayo ndio msingi wa mustakabali wa nchi yao. Hali hii inaweza kusababisha watu au makundi yanayopenda kushiriki katika kujadili katiba pendekezwa kutojitokeza tena kwa hofu ya kufanyiwa fujo.

Aidha, kuhusu kufanyiwa fujo kwa aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya mabadiliko ya Katiba Jaji mstaafu Joseph Warioba, na watu wengine akiwemo mwanamke na mlemavu wa macho waliokuwa wanashiriki katika mjadala huo, kitendo hicho ni cha kidhalilishaji kinacholenga kufifisha maoni ya wananchi. FemAct ikiwa ni muungano wa watetezi wa haki za kijamii tunaamini kuwa mtu yeyoye ana uhuru wa kutoa maoni yake na kusikilizwa na watu wengine bila kufanyiwa vurugu, kudhalilishwa au kudhuriwa kwa namna yoyote.

Hofu yetu ni kwamba matukio kama haya yanawatisha wanawake , makundi yaliyoko pembezoni, na hasa walemavu kushiriki katika hatua zinazofuata ikiwemo uchaguzi wa serikali za mitaa, kura za maoni na uchaguzi mkuu 2015 kikamilifu kwasababu watahofia kufanyiwa vurugu.

Kwa takribani miaka 10 iliyopita tumeshuhudia idadi ya wapiga kura nchini ikizidi kushuka badala ya kuongezeka licha ya kuwa idadi ya watu nchini kuongezeka. Sababu kama hizi za kuvuruga amani katika mikusanyiko ya wananchi,na mikutano ambayo wananchi wanapashana taarifa inafifisha ari ya wananchi kujitokeza na kutoa michango yao kidemokrasia.

Ili kuhakikisha mchakato huu unafanyika katika hali stahiki, na wananchi kushiriki kikamilifu chaguzi zinazokuja, FemAct inapendekezakuzingatiwa kwa masuala yafuatayo;

    Uhuru wa wananchi wa Tanzania wa kujieleza na kutoa maoni yao , uheshimiwe katika kujadili mambo yanayohusu mustakabali wa nchi yao ikiwemo katiba inayopendekezwa na makundi yote yakiwemo yaliyoko pembezoni yapewe nafasi na kuhakikishiwa usalama.


    Vyombo vya usalama vihakikishe kuwa, usalama unakuwepo kwa wananchi muda wote wanaposhiriki katika mchakato wa kujadili na kupiga kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa pamoja na chaguzi zijazo.


    Vijana ambao ni zaidi ya asilimia 65% ya idadi ya watu/watanzania nchini, waepuke kutumiwa na watu binafsi, vyama vya siasa au makundi fulani katika jamii ili kuepukana na kuharibika kwa hali ya usalama katika nchi yetu.


    Vyama vya siasa au makundi yoyote kuacha mara moja kushiriki katika vitendo vya kiuchochezi au vinavyoweza kusababisha vurugu katika nchi yetu.


5. Wananchi waachwe wajadili kwa mapana maudhui ya Katiba inayopendekezwa bila kuwekewa mipaka au ukomo ili waielewe kabla ya kushiriki upigaji kura kama ilivyopendekezwa.

Lilian Liundi
Kaimu Mkurugenzi Mtandaji -TGNP Mtandao








All the contents on this site are copyrighted ©.