2014-11-10 11:16:18

Marehemu Rais Sata, "King Cobra" atakumbukwa na wengi!


Rais Michael Chilufya Sata wa Zambia aliyefariki dunia kunako tarehe 28 Oktoba 2014 huko London Uingereza anazikwa tarehe 11 Novemba 2014 kwenye Makaburi ya Taifa yaliyoko kwenye Uwanja wa Mabalozi, mjini Lusaka. Mazishi haya yatatanguliwa na Ibada ya Misa takatifu, itakayoadhimishwa kwenye Uwanja wa Mashujaa wa Zambia na baadaye maziko yatafuatia.

Katika kipindi cha majuma mawili ya maombolezo wananchi wa Zambia pamoja na watu wenye mapenzi mema wamemkumbuka kwa sala na ibada mbali mbali, ili kumwombea pumziko la uzima wa milele. Wananchi wa Zambia wanaoishi mjini Roma na katika viunga vyake, Jumapili tarehe 9 Novemba 2014 wameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumwombea Marehemu Rais Sata wa Zambia, aliyefahamika na wengi kama "King Cobra".

Ibada hii ya Misa takatifu imeongozwa na Padre Paul Samasumo, Mkuu wa Idara ya Kiingereza ya Radio Vatican aliyefafanua kuhusu Fumbo la Kifo katika maisha ya mwanadamu, akiwataka waamini na watu wenye mapenzi mema waliohudhuria katika Ibada hii ya Misa Takatifu kujiandaa kikamilifu ili kukabiliana na Fumbo la Kifo, kwani hawajui siku wala saa watakapokutana na kifo. Lakini jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, walau wanakumbukwa.

Padre Samasumo anasema, Marehemu Rais Sata atakumbukwa na wengi kwamba alikuwa ni mchapakazi, mzalendo na mnyenyekevu, mtu aliyekubali kushindwa na kusonga mbele kwa imani na matumaini. Hakuwa ni mtu aliyetaka kung'ang'ania madaraka hata kwa gharama ya maisha ya wananchi wa Zambia. Amewataka wananchi wa Zambia kuendelea kusali kwa ajili ya amani na utulivu wakati huu wa kipindi cha mabadiliko kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika katika kipindi cha siku tisini.

Rais Guy Scott anasema, angependa kukumbukwa kwamba, ameiongoza Zambia kwa amani na utulivu na kufanikisha mchakato wa uchaguzi mkuu kadiri ya Katiba ya nchi na wala si vinginevyo.







All the contents on this site are copyrighted ©.