2014-11-10 09:57:12

Hakuna amani pasipo na maendeleo ya kweli!


Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya limeitaka Serikali kuchukua maamuzi machungu kwa kufanya mabadiliko makubwa katika vyombo vya ulinzi na usalama baada ya askari 20 kuuwawa kikatili na kikundi cha majambazi, huko Turkana. Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki anasema, ukweli utawaweka huru na kwamba, jamii haiwezi kuvumilia kuona usaliti ukifanywa na watu waliopewa dhamana ya kulinda usalama wa raia na mali zao na kwamba, vitendo kama hivi si mara ya kwanza vinajirudia nchini Kenya.

Kuna vitendo vya uhalifu vinavyopelekea watu kupoteza maisha na mali zao, lakini mkondo wa sheria umekuwa unasuasua kuchukua hatua madhubuti, kiasi kwamba, watu wanaanza kukosa imani na vyombo vya ulinzi na usalama.

Baraza la Maaskofu linaitaka Serikali kuachana na maneno, na kuanza kutekeleza sera zake kwa vitendo, ili kulinda haki, amani na ustawi wa wananchi wa Kenya. Katiba ambayo ni Sheria mama iwalinde wanachi na Serikali ijitahidi kuwapatia huduma msingi kwani hadi sasa hata baada ya miaka 50 ya Uhuru wa Kenya, kuna miji ambayo imesahaulika katika mchakato wa maendeleo.

Baraza la Maaskofu katika tamko lao, lina sema, hakuna amani ya kweli pasi na maendeleo endelevu ya watu. Maaskofu wanaiomba Serikali kushughulikia kwa kina na mapana maeneo yote ya ardhi yenye umiliki wa utata hasa katika maeneo ambayo yana utajiri mkubwa wa madini ili haki iweze kutendeka na hatimaye, kuondoa kinzani za kijamii zinazokwamisha mchakato wa maendeleo endelevu.







All the contents on this site are copyrighted ©.