2014-11-08 15:06:14

Waonesheni vijana kwamba ninyi ni Wamissionari wa matumaini na furaha!


Watawa wanaalikwa na Mama Kanisa kushiriki kikamilifu katika majiundo ya vijana wa kizazi kipya kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji, kwani vijana wanapambana na changamoto mbali mbali katika maisha yao, hasa kutokana na umaskini wa maisha ya kiroho na kiutu; vijana wanapungukiwa na upendo pamoja na mahusiano thabiti ya kijamii.

Baba Mtakatifu Francisko ameyasema hayo, Jumamosi tarehe 8 Novemba 2014, wakati alipokutana na kuzungumza na wajumbe wa mkutano mkuu wa Shirika la Masista wa Bikira Maria msaada wa daima. Baba Mtakatifu amewataka watawa hawa kuiga mfano wa Mtakatifu Yohane Bosco na Mama Mazzarello, kwa kuwaonjesha vijana ujumbe unaofumbatwa katika upendo na huruma ya Mungu kwa kila binadamu.

Baba Mtakatifu anawataka watawa hawa kutoka na kuwaendelea watu wanaoishi pembezoni mwa Jamii kijiografia pamoja na kukosa mahitaji yao msingi kama binadamu; kwa kutoa upendeleo wa pekee kwa maskini na wote wanaotengwa kutokana na hali yao ya maisha.

Watawa wayasimike maisha yao katika mabadiliko, toba na wongofu wa ndani unaojidhihirisha katika utekelezaji wa mikakati ya shughuli za kichungaji, hili nyumba zao ziweze kuwa kweli ni mazingira ya Uinjilishaji kwa kuwashirikisha vijana katika utume na maisha ya Kanisa. Wanapaswa kuwajibika kwa kuwasaidia vijana katika hija ya maisha yao ya kiimani, ili hatimaye, vijana wenyewe waweze kushikamana na Yesu na kuwa ni vyombo vya Uinjilishaji kwa vijana wenzao.

Watawa waendelee kusikiliza sauti ya Roho Mtakatifu pamoja na kupokea neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu pamoja na kutambua mahitaji msingi ya binadamu na kizazi ambacho kinakumbana na mabadiliko makubwa. Waoneshe ushuhuda wa kinabii katika sekta ya elimu, ukarimu kwa vijana huku wakikabiliana na changamoto za mwingiliano wa tamaduni, ili kupambanua njia muafaka zinazoweza kutumiwa katika shughuli zao za kichungaji katika maisha ya vijana wanaoendelea kuogelea katika ulimwengu wa mitandao na maendeleo ta teknolojia ya digitali.

Baba Mtakatifu anasema, ili kuweza kufanikisha mikakati hii, kuna haja kwanza kabisa kumweka Yesu Kristo kuwa ni kiini cha maisha yao, huku wakiongozwa na Neno la Mungu linalowaongoza katika mikakati ya kimissionari pamoja na kudumu katika maisha ya sala; ushuhuda wa maisha ya kidugu na kupokeana kama walivyo ili kukuza na kudumisha karama na zawadi ambazo Mwenyezi Mungu amemkirimia kila mmoja wao, ili kuonesha kweli kwamba, wao ni Wafuasi waYesu, jambo linalohitaji majiundo makini katika maisha ya kitawa yanayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili, pamoja na kuendelea kusoma alama za nyakati, ili kumwilisha kikamilifu ujumbe wa Injili pamoja na kujisadaka kwa upendo.

Baba Mtakatifu amegusia mambo msingi waliyojadili wakati wa maadhimisho ya mkutano mkuu wa Shirika, kwa kuonesha furaha, majonzi na wasi wasi; pamoja na matarajio ya watu wanaowahudumia. Wanapaswa kushikamana na vijana, watoto na wanawake kadiri ya hali na mazingira yao, ili kuwaonesha kwamba, wao kweli ni wamissionari wa matumaini na furaha, huku wakionesha tunu msingi za maisha ya watoto wa Mtakatifu Bosco; yaani upendo kwa Mungu na vijana. Katika shida na mahangaiko kamwe wasikate tamaa, bali waendelee kujielekeza zaidi na zaidi katika mchakato wa Uinjilishaji mpya kwenye sekta ya elimu, katekesi na majiundo makini kwa vijana.

Baba Mtakatifu Francisko, mwishoni, amekazia umuhimu wa maisha ya kijumuiya kama sehemu ya utekelezaji wa utume wao ndani ya Kanisa, kwa kushuhudia kwamba, kweli wanajisadaka kwa ajili ya Mungu na jirani.







All the contents on this site are copyrighted ©.