Askofu mkuu mstaafu James Mwewa Spaita wa Jimbo kuu la Kasama amefariki dunia!
Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA limetuma
salam za rambi rambi kwa Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia kutokana na msiba wa Askofu
mkuu mstaafu James Mwewa Spaita, 80, aliyefariki tarehe 4 Novemba 2014 na kuzikwa
tarehe 7 Novemba 2014, katika Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane, Jimbo kuu la Kasama.
Padre
Ferdinandi Lugonzo, Katibu mkuu wa AMECEA anasema, Marehemu Askofu mkuu mstaafu James
Mwewa Spaita atakumbukwa na wengi kutokana na huduma za kichungaji alizozitoa kwa
Familia ya Mungu nchini Zambia na katika nchi za AMECEA kwa ujumla wake.
Marehemu
Askofu mkuu Spaita alizaliwa kunako tarehe 8 Aprili 1934 huko Bombwe. Baada ya masomo
na majiundo yake ya kikasisi, akapadrishwa kunako tarehe 9 Septemba 1962. Tarehe 28
Februari 1974 akateuliwa kuwa ni Askofu wa Jimbo Katoliki la Mansa, Zambia na kuwekwa
wakfu hapo tarehe 28 Aprili 1974. Tarehe 3 Desemba 1990, Baba Mtakatifu Yohane Paulo
II akamteuwa kuwa ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Kasama na kung'atuka kutoka madarakani
kadiri ya sheria za Kanisa hapo tarehe 30 Aprili 2009. Apumzike kwa Amani. Amina.