2014-11-07 08:36:19

Ni kwa ajili ya mafao ya familia!


Kardinali Lorenzo Baldisseri, Katibu mkuu wa Sinodi za Maaskofu anasema kwamba, maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya familia, ambao muhtasari wake umewekwa kwenye Hati ya Mababa wa Sinodi inayojulikana kama "Relatio Synodi" itakayotumiwa wakati wa maadhimisho ya Sinodi ya Kawaida ya Maaskofu kuanzia tarehe 4 hadi tarehe 25 Oktoba 2015 inaonesha wito, utume na dhamana ya Mama Kanisa katika mchakato wa kutangaza Injili ya Familia kwa Watu wa Mataifa.

Hii ni changamoto kwa Makanisa mahalia kuendelea kukazia tunu msingi za maisha ya ndoa na familia mintarafu sheria, kanuni na Mapokeo ya Mama Kanisa. Hati hii inaonesha changamoto mintarafu Mafundisho ya Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican pamoja na Mapokeo ya Kanisa kadiri yalivyofafanuliwa na viongozi wa Kanisa kwa nyakati mbali mbali, ili kukuza na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, kama nguzo thabiti za ujenzi wa Familia kama Kanisa dogo la nyumbani.

Familia inapaswa kuwa ni shule ya utu na heshima ya binadamu; kitalu cha Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili na kwamba, Familia ni Kanisa dogo, linalotoka kuwaendelea Watu wa Mataifa ili kushuhudia kwa njia ya maneno na mifano adili ya maisha, Injili ya Familia. Ili kufikia lengo hili, Familia hazina budi kutekeleza dhama yake msingi ya malezi na majiundo kwa watoto na vijana wa kizazi kipya, kwa kuwashirikisha mang'amuzi ya maisha yanayojikita katika uzoefu wa imani na tunu msingi za maisha ya ndoa na familia. Wanafamilia wanahamasishwa kuwa kweli ni shule ya upendo na huruma, kwa kusaidiana, kufarijiana na kutaabikiana katika safari ya maisha ya kila siku.

Mababa wa Sinodi katika majadiliano yao wamekiri kwamba, Familia ni mahali ambapo wanafamilia wanajifunza kujenga na kudumisha mahusiano ya kijamii, kumbe Familia ni shule ya mahusiano ya kijamii, ni shule maisha na utume wa Kanisa; ni madhabahu ya zawadi ya maisha, mahali ambapo maisha yanalindwa na kuendelezwa katika hatua mbali mbali. Hapa familia inakumbushwa kwamba ni sehemu muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa, dhamana inayotekelezeka kwa njia ya majiundo makini ya watoto katika masuala ya kiimani, kiutu na kitamaduni.

Mababa wa Sinodi wamewataka wanafamilia kuhakikisha kwamba, wanajenga na kudumisha mahusiano kati ya vijana wa kizazi kipya na wazee ambao ni "Maktaba rejea" ya tunu msingi za maisha ndani ya jamii; bila kusahau kwamba, kwa njia ya Sakramenti ya ndoa, Bwana na Bibi wanaunga na kuwa ni mwili mmoja, tukio ambalo pia linaunganisha familia mbili tofauti na hivyo kuanza kutembea kwa pamoja na katika mshikamano wa upendo.

Kuna hatua kubwa ambayo imefikiwa na Jumuiya ya Kimataifa katika kukuza na kudumisha haki msingi za binadamu, uhuru na utu wa binadamu. Lakini kwa upande mwingine ni mambo ambayo yanapaswa kuangaliwa kwa umakini mkubwa, ili haki binafsi zisiharibu tunu msingi za maisha ya ndoa na familia kwa kutaka kuhalalisha hata mambo yale ambayo kimsingi ni dalili za kumong'onyoka kwa utu na heshima ya binadamu; upweke hasi na mahusiano tenge kati ya watu.

Mababa wa Sinodi wanabainisha kwamba, licha ya mapungufu haya ya kibinadamu, Kanisa kwa upande wake linapenda kusimama kidete kulinda na kutetea tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, kwa ajili ya mafao na ustawi wa familia ya binadamu pamoja na kuziwezesha familia kutekeleza dhamana ya kutoa majiundo makini kwa watoto wao.

Mama Kanisa anaangalia haki na huruma kama mambo ambayo yanaweza kusaidia kukuza maisha ya ndoa na familia. Mafao ya Familia hayana budi kumwilishwa katika uhalisia wa maisha, vinginevyo yataendelea kuelea katika ombwe, bila kuwa na mafao kwa familia zenyewe. Kardinali Lorenzo Baldisseri anasema, Kanisa katika maadhimisho ya awamu ya kwanza ya Sinodi kwa ajili ya familia limeanza safari ndefu ya kutangaza Injili ya Familia, safari inayohitaji mchango wa hali na mali kutoka kwa kila familia!







All the contents on this site are copyrighted ©.