2014-11-07 08:04:34

Mambo ya Kale ni ushuhuda wa maisha na utume wa Kanisa!


Roma ni mji ambao unahifadhi kumbu kumbu nyingi za kihistoria, mambo ambayo yana utajiri mkubwa katika historia, maisha na utume wa Kanisa. Ni mahali ambapo kuna chimbuko la imani na tamaduni ambazo zimesaidia kuleta mchakato wa mabadiliko katika maisha ya mwanadamu: kiroho, kimwili na kitamaduni.

Ni mji unaonesha shuhudi za imani zilizotolewa na miamba wakuu wa Kanisa kama vile Mtakatifu Petro na Paulo, ambao kwa njia ya ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, leo Kanisa limeenea sehemu mbali mbali za dunia. Kanisa limeendelea kuwaenzi wafiadini, waliojisadaka maisha yao kwa kutunza kwa heshima kubwa makubiri yanayopatikana mjini Roma. Hawa ni vielelezo vya imani ya Kanisa kuhusu mateso, kifo na ufufuko wa Yesu, unaowakarimia waamini maisha mapya yanayofumbata uzima wa milele.

Hii ni sehemu ya hotuba iliyotolewa na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, Alhamisi, tarehe 6 Novemba 2014, wakati wa kuzindua Mwaka wa Masomo wa Taasisi ya Kipapa ya Mambo ya Kale. Watu wanahimizwa kutunza utajiri huu kwa ajili ya mafao ya kizazi kijacho na kwamba, Papa Pio wa kumi na moja aliona umuhimu wa utunzaji za kumbu kumbu za kale ndiyo maana akaanzisha taasisi ya kipapa kwa ajili ya mambo ya kale, ambayo yana maana sana katika maisha na utume wa Kanisa.

Hii ni taasisi ambayo inatoa masomo kwa vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wanaofika hapo ili kujifunza kwa kina na mapana jinsi ya mambo ya kale; kwa kuona kwa macho yao wenyewe pamoja na kushiriki katika makongamano mbali mbali ya kitaifa na kimataifa, mambo msingi kama sehemu ya mchakato endelevu wa kitaaluma. Kardinali Pietro Parolin anawatakia wote heri na fanaka katika masomo na maisha yao ya kila siku.







All the contents on this site are copyrighted ©.