2014-11-06 09:00:35

Mwongozo kwa Makardinali na Maaskofu kung'atuka kutoka madarakani


Baba Mtakatifu Francisko katika mazungumzo yake na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican hapo tarehe 3 Novemba 2014, amemruhusu achapishe kanuni zitakazotumika kwa ajili ya Maaskofu wa Jimbo na viongozi wote wa Kanisa wanaoteuliwa na Khalifa wa Mtakatifu Petro kushika nyadhifa mbali mbali ndani ya Kanisa.

Baba Mtakatifu anawaalika kwa namna ya pekee, wahusika kuhakikisha kwamba, wanafuata sheria na kanuni zilizopo kwa kutambua kwamba, Uaskofu ni huduma na wala si cheo. Maaskofu wanapaswa kuandika barua ya kung'atuka kutoka madarakani wanapotimiza umri wa miaka 75. Ombi hili linapokubaliwa na Baba Mtakatifu, madaraka yote aliyo nayo mhusika hata katika ngazi ya kitaifa yanasitishwa mara moja.

Katika mwelekeo huu, Familia ya Mungu inachangamotishwa kwa namna ya pekee kabisa kuonesha moyo wa upendo na mshikamano kwa aliyekuwa kiongozi wa maisha yao ya kiroho, kwa kuzingatia kanuni ya haki na upendo. Katika mazingira maalum, viongozi wanaohusika wanaweza kumwomba Askofu kuandika barua ya kung'atuka kutoka madarakani, baada ya kumsikiliza kwa umakini mkubwa na katika majadiliano ya kidugu.

Makardinali na wakuu wa Taasisi za Kipapa pamoja na Makardinali wanaotekeleza dhamana yao kwa kuteuliwa na Khalifa wa Mtakatifu Petro; watatakiwa wafikishapo umari wa miaka 75 kuwasilisha ombi la kung'atuka kutoka madarakani kwa Baba Mtakatifu, atakayetolea maamuzi kwa wakati wake. Wakuu wa Mabaraza na Taasis za Kipapa, Makatibu wakuu na Maaskofu wanaotekeleza dhamana yao kwa uteuzi wa Baba Mtakatifu, dhamana yao ufika ukomo wanapotimiza umri wa miaka 75; wajumbe wanapotimiza umri wa miaka 80 dhamana na huduma yao inasitishwa mara moja.







All the contents on this site are copyrighted ©.