2014-11-06 11:51:56

Mkimbilieni Mwenyezi Mungu ili muonje huruma na upendo wake katika Sakramenti ya Upatanisho!


Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican, Alhamisi tarehe 6 Novemba 2014 amewataka Wakristo kuonesha moyo wa toba kwa kukimbilia Sakramenti ya Upatanisho, ili kuonja huruma na upendo wa Mungu unaotolewa na Mama Kanisa kwa njia ya Wahudumu wa Injili, ili waweze kujipatia wokovu na uzima wa milele.

Baba Mtakatifu anasema inasikitisha kumwona Padre akiwa amefungua mlango wa Kanisa na kuendelea kusubiri waamini kuja kuungama na hakuna anayejitokeza, lakini mbaya zaidi kwa waamini ambao hawaoni tena sababu ya kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu. Viongozi wa Kanisa hawana budi kuhakikisha kwamba, wanajitahidi kadiri ya uwezo wao kuwaganga wale waliovunjika moyo bila ya kukata tamaa kwa kutambua kwamba, Mwenyezi Mungu anapenda kila mtu aweze kuokoka na kupata uzima wa milele.

Yesu Kristo aliyamimina maisha yake kwa ajili ya kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti, changamoto na mwaliko kwa viongozi wa Kanisa kutoogopa kuwaendelea na kuwahudumia wadhambi, ili waonje huruma na upendo wa Mungu katika maisha yao. Kanisa linawahitaji viongozi wema na watakatifu, linataka kuwaona Wakristo wema na watakatifu pia, ili kwa pamoja waweze kumwomba na kumwabudu Mwenyezi Mungu, kwa kuwatangazia wengine Habari Njema ya Wokovu.







All the contents on this site are copyrighted ©.