2014-11-06 14:37:47

Mambo ya kuzingatia katika kupambana na baa la umaskini duniani!


Jumuiya ya Kimataifa katika kipindi cha miaka kumi, yaani kuanzia mwaka 2008 hadi mwaka 2017 ilijiwekea mkakati wa kupambana na baa la umaskini duniani, utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia sanjari na kuweka sera bora za maendeleo endelevu. Hii ni changamoto endelevu kwa Jumuiya ya Kimataifa kutokana na ukweli kwamba, bado baa la umaskini linaendelea kuyaandama mallioni ya watu duniani. RealAudioMP3

Sera na mikakati ya mapambano dhidi ya umaskini wa hali na kipato zizingatie kwa namna ya pekee hali halisi, uzoefu na mang’amuzi ya watu kuliko mtindo wa sasa wa kutoa sera ambazo zimekwisha andaliwa kwenye maabara ambazo hazitekelezeki na matokeo yake watu wanaendelea kuogelea katika dimbwi la umaskini. Sera makini na siasa bora ni nyenzo msingi katika mapambano dhidi ya baa la umaskini, kwa kuwahusisha watu wenyewe pamoja na kujenga mshikamano wa dhati ndani ya Jamii.

Ni changamoto iliyotolewa hivi karibuni na Askofu mkuu Bernaditto Auza, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa wakati akichangia hoja kwenye Baraza kuu la Umoja wa Mataifa, lililokuwa linajadili mikakati ya kupambana na baa la umaskini duniani. Maendeleo ya kweli yanajikita katika sera makini zinazowahusisha wadau katika medani mbali mbali za maisha, sanjari na kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu kama mlengwa mkuu wa maendeleo.

Askofu mkuu Auza anasema, sera nyingi zilizoibuliwa na Jumuiya ya Kimataifa katika mapambano dhidi ya baa la umaskini, bado hazijaonesha mafanikio makubwa, kwani watu wanaendelea kutumbukia katika umaskini wa hali na kipato, mambo yanayo nyanyasa utu na heshima ya binadamu. Wanawake wanapaswa kupewa fursa na haki sawa katika mchakato wa utekelezaji wa sera na mikakati ya maendeleo kwani katika sehemu nyingi duniani wanawake “ ni majembe” ya mandeleo.

Na takwimu zinaonesha kwamba, waathirika wakubwa wa balaa la umaskini ni wanawake na watoto; hali ambayo inachangiwa kwa kiasi kikubwa na ubaguzi katika utoaji wa huduma msingi za kijamii kama vile elimu, afya, utamaduni, kisiasa na mwelekeo wa maisha ya kiroho.

Ikumbukwe kwamba, mchakato wa kupambana na baa la umaskini haulengi kuwaongezea watu fedha mifukoni, bali ni kuhakikisha kwamba, mtu mzima anakombolewa kutoka katika umaskini na hivyo kumwezesha kupata ustawi na maendeleo ya kweli: kiroho na kimwili; changamoto kwa kila mtu kuchangia ili kweli Jumuiya ya Kimataifa iweze kufikia lengo hili linalopania kuwafaidia wengi kwa kuongozwa na kanuni ya mshikamano.








All the contents on this site are copyrighted ©.