Rais JK. achonga na wazee wa Dodoma kuhusu masuala nyeti ya kitaifa!
Ifuatayo ni hotuba ya Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania, wakati akizungumza na wazee
wa Dodoma, Jumanne tarehe 4 Novemba 2014 kuhusu masuala mbali mbali ya kitaifa na
kimataifa!
Ndugu Wananchi; Nakushukuru sana Mwenyekiti wa Baraza la Wazee
wa Dodoma, Mheshimiwa Balozi Job Lusinde kwa kuandaa mkutano huu. Wakati nilipofanya
ziara ya Mkoa wa Dodoma tulipanga tukutane lakini kwa vile ratiba yangu iliingiliwa
na mambo mengi, hivyo haikuwezekana, lakini leo imewezekana. Pengine hii ndiyo siku
ambayo Mwenyezi Mungu alipanga tukutane.
Tumshukuru Muumba wetu kwa rehema
zake, na tumuombe ajaalie mkutano wetu uanze salama na uishe salama. Nawashukuru kwa
Risala yenu na maudhui yake. Nawaahidi nitayafuatilia na majibu mtapata. Pamoja na
yaliyomo kwenye risala yenu mimi nina mambo manne ambayo ni yatokanayo na ziara yangu
nchini China na Vietnam, maradhi ya Ebola, uchaguzi wa Serikali za Mitaa na hatua
zinazofuata kwenye Mchakato wa Katiba.
Ziara ya China na Vietnam Ndugu
Wananchi; Kuanzia tarehe 21 Oktoba, 2014 hadi tarehe 28 Oktoba, 2014 nilikuwa katika
ziara rasmi ya kutembelea nchi za China na Vietnam. Nilitembelea China tarehe 21 hadi
26 Oktoba, 2014 na Vietnam tarehe 26 hadi 28 Oktoba, 2014. Ziara hizo nilizifanya
kufuatia mwaliko wa Rais wa China, Mheshimiwa Xi Jinping na mwaliko wa Rais wa Vietnam
Mhe. Truong Tan Sang. Ziara katika nchi hizo zilikuwa za mafanikio makubwa sana hata
kuliko nilivyotarajia. Nchini China tulipokelewa kwa namna hawajafanya kwa miaka mingi.
Ziara
ya China Ndugu Wananchi; Nchini China, kwa makubaliano na wenyeji wetu tulifanya
hafla maalum ya kuadhimisha miaka 50 tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia
kati ya Tanzania na China. Katika hafla hii upande wa China uliwakilishwa na Makamu
wa Rais Mheshimiwa Li Yuanchao. Pande zetu mbili ziliitumia fursa hiyo kuzungumzia
tulipotoka, tulipo sasa na mbele tuendako.
Kwa jumla wote tumeridhika kuwa
tumekuwa na nusu karne ya uhusiano wenye mafanikio makubwa. Katika kipindi hiki nchi
zetu zimekuwa marafiki wa kweli, wa kuaminiana na kusaidiana kwa mambo mengi. Katika
medani za kimataifa nchi zetu zimekuwa zikielewana kwa mambo mengi na kusaidiana.
China ilikuwa ngome kuu katika kusaidia kwa hali na mali harakati za ukombozi wa Kusini
mwa Afrika.
Wakati ule Tanzania ilikuwa ikiongoza nchi za mstari wa mbele.
Wenzetu bado wanakumbuka sana jinsi nchi yetu ilivyokuwa mstari wa mbele kuipigania
nchi ya China kurejeshewa haki yao hususan ya kuketi kiti chao katika Umoja wa Mataifa,
baada ya Chama cha Kikomunisti chini ya uongozi wa Mwenyekiti Mao Tse Tung kufanikiwa
kukishinda Chama cha Kuomintang na kiongozi wake Chian Kai Sheki na kulazimika kukimbilia
Taiwan. Mataifa makubwa ya Magharibi yalikataa kuitambua China mpya na kuitenga. Katika
kufanya hivyo, waliitambua Taiwan na kuifanya kuwa ndiyo wawakilishi wa China katika
Umoja wa Mataifa.
Baada ya hapo Jamhuri ya Watu wa China ilipinga uamuzi ule
na kuanzisha kampeni ya kudai haki yake stahiki. Madai yao hayo yalipata nguvu pale
Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere alipoamua kuwa Tanzania ishiriki katika kampeni
hiyo kwa nguvu zake zote. Kwa kushirikiana na nchi nyingine rafiki, jitihada hizo
za pamoja zilizaa matunda na mwaka 1971, China ilipokubaliwa kuchukua nafasi yake
stahiki katika Umoja wa Mataifa na Taiwan kuondolewa.
Ndugu zetu wa China
hawasahau msaada wetu huo na hawaoni haya kulisemea waziwazi jambo hilo na vizazi
vyote vya China vinafundishwa kuhusu wema ambao Tanzania imewafanyia. Kwa sababu hiyo,
Tanzania ina nafasi maalum nchini China. Wao wenyewe wana msemo maalumu kuhusu Tanzania
kwamba ni “all weather friends”. Yaani marafiki wa majira yote.
Katika ziara
yangu nilifuatana na kaka yangu Dkt. Salim Ahmed Salim ambaye ndiye alikuwa Balozi
wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa wakati ule. Rafiki zetu wa China walifurahi
sana kumwona Dkt. Salim kwani yeye hasa ndiye aliyefanya kazi ya kushawishi nchi nyingine
kuiunga mkono Jamhuri ya Watu wa China. Pia nilifuatana na Mheshimiwa Balozi Mstaafu
Jenerali Mrisho Sarakikya aliyekuwa Mkuu wa Majeshi wa kwanza wa Tanzania. Yeye ndiye
alihusika sana kujenga uhusiano wa mambo ya kijeshi baina ya nchi yetu na China. Pia,
nilikwenda na Balozi Mstaafu, Mzee Waziri Juma aliyewahi kuwa Balozi wa Pili wa Tanzania
nchini China.
Kama mjuavyo nchi ya China imetusaidia mambo mengi kwa maendeleo
yetu. Misaada mingine ilihusu vitu vikubwa ambavyo katika hali ya kawaida isingewezekana
kusaidiwa na nchi nyingine zinazotoa misaada ya maendeleo na mikopo. Miongoni mwa
hayo ni ujenzi wa Reli ya Uhuru (TAZARA), misaada ya zana, vifaa na mafunzo vilivyosaidia
kujenga Jeshi letu jipya yaani JWTZ baada ya kuvunjwa kwa lile tulilorithi kutoka
kwa Wakoloni kuaasi Januari 20, 1964. Msaada wao mkubwa ndiyo uliotuwezesha mpaka
kuweza kulinda na kukomboa nchi yetu dhidi ya uvamizi na kutekwa eneo la Misenyi,
Kagera na majeshi ya dikteta Iddi Amin wa Uganda.
Hata sasa China imeendelea
kuwa mshirika wetu mkubwa kuliko wote katika kuimarisha na kuendeleza Jeshi letu.
Msaada mwingine mkubwa ni ule mkopo wa dola za Marekani bilioni 1.2wa kujenga bomba
jipya la gesi kutoka Mtwara na Songosongo hadi Dar es Salaam. Isingekuwa rahisi kupata
mkopo mkubwa kiasi kile kutoka nchi nyingine au Shirika lolote la fedha duniani. Mkopo
ule unalimaliza tatizo la upungufu wa umeme kutokea sasa mpaka mwaka 2020 inapokadiriwa
kuwa nchi yetu itahitaji megawati 10,000. Hata wakati huo bomba hili ni muundombinu
wa msingi utakaorahisisha upanuzi wa miundombinu ya kuzalisha umeme kutosheleza mahitaji
hayo kama itaamuliwa gesi iendelee kuwa chanzo kikuu cha nishati ya umeme nchini.
Katika
mazungumzo yangu na Waziri Mkuu Li Keqiang na Rais Xi Jinping wote wawili wameelezea
kuridhika kwao na uhusiano baina ya nchi zetu tangu siku za nyuma mpaka hapa tulipo
sasa. Hali kadhalika walielezea kuwa wangependa kuona uhusiano wetu na ushirikiano
wetu unaimarika na kukua mpaka kufikia hatua bora na ya juu kabisa. Niliwahakikishia
kuwa hiyo ndiyo fikra yangu na Watanzania kuhusu uhusiano baina ya nchi zetu mbili
rafiki.
Kwa nyakati tofauti viongozi wote wakuu wa China walinihakikishia utayari
wao wa kuendelea kuchangia maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kiusalama ya Tanzania.
Jambo lililonipa faraja kubwa mimi na wenzangu ni kuwa mambo yote tuliyoomba ndugu
zetu wa China watusaidie wamekubali. Hakika Wachina wameendelea kuwa marafiki wa kweli
wa nchi yetu na watu wake.
Tuliwaomba waendelee kushirikiana nasi na wabia
wenzetu wa Zambia kulijenga upya Shirika la Reli ya TAZARA na wamekubali. Tuliwaomba
pia tuendelee kushirikiana kukuza uwekezaji na biashara baina ya nchi zetu mbili rafiki.
Walilipokea jambo hilo kwa furaha. Ni ukweli ulio wazi kwamba biashara na uwekezaji
umekua sana kiasi cha kuifanya China kuwa nchi inayoongoza kwa mambo yote mawili.
Hata hivyo, sote tumekubaliana kuwa biashara ya dola za Marekani bilioni 3.7 na uwekezaji
wa dola za Marekani bilioni 2.5 ni kidogo mno hivyo tuongeze juhudi tufanye vizuri
zaidi katika kipindi kifupi kijacho.
Ndugu Wananchi; Kulikuwa na mkutano
mkubwa wa uwekezaji uliohudhuriwa na makampuni ya kichina yapatayo 500 yaliyokuwa
tayari kuwekeza na kufanya biashara na Watanzania. Kwa upande wetu miradi kadhaa tuliyopeleka
imepata wabia. Miongoni mwa waliofaninikiwa sana ni Shirika la Nyumba la Taifa waliopata
wabia watakaowekeza dola za Marekani bilioni 1.7 kwenye ujenzi wa nyumba.
Aidha,
kuhusu ujenzi wa Ukanda wa Kiuchumi wa Mbegani ambao tuliwaomba watusaidie kusukuma
utekelezaji wake, viongozi wa China walielezea utayari wao kusaidia mradi huo ufanikiwe.
Tulipokuwa Shenzhen, tulipata nafasi ya kutembelea Makao Makuu ya Kampuni ya China
Merchants Ltd., na kuzungumza na viongozi wake. Walitembezwa kuangalia shughuli za
kampuni hiyo ikiwa ni pamoja na jinsi Kampuni hiyo ilivyoshiriki katika ujenzi wa
mji wa Shenzhen kutoka kijiji cha uvuvi na kuwa jiji kubwa la kisasa, lenye maendeleo
ya kiuchumi, teknolojia na biashara. Waliahidi kutumia ujuzi wao, maarifa yao na uwezo
wao wa kifedha kujenga Mbegani kama ilivyotokea Shenzhen.
Siku ile pia tulishuhudia
Mfuko wa Akiba wa Oman wakitiliana saini na China Merchants na Mamlaka yetu ya Uendeshaji
wa Maeneo Huru ya Uwekezaji (EPZA) hati ya makubaliano kujiunga rasmi katika kuwekeza
na kushiriki katika utekelezaji wa mradi huo. Kilichonifurahisha sana siku ile ni
kule kuwepo kwa mpango kazi unaotarajia ujenzi wa bandari na ukanda wa maendeleo ya
kiuchumi wa Mbegani kuanza tarehe 1 Julai, 2015.
Hali kadhalika, nilipokuwa
Shenzhen nilipata nafasi ya kutembelea kampuni za teknolojia ya habari na mawasiliano
za Huawei na ZTE. Nilifika mjini Jinan, Jimbo la Shandong na kutembelea kampuni nyingine
kubwa ya aina hiyo iitwayo INSPUR. Bahati nzuri kampuni zote zimewekeza Tanzania na
wanataka kupanua uwekezaji wao.
Nilipokuwa Jinan nilitembelea Hospitali Kuu
ya Jimbo la Shandgon, Mjini Jinan, ambayo imetoa madakatari wengi na kupata nafasi
ya kuwashakuru viongozi wa Jinan na Jimbo la Shandong kwa kutuletea madakatari na
wataalamu wengine wa afya kuja kufanya kazi nchini Tanzania. Vile vile, nimewashukuru
kwa mchango wao muhimu uliotuwezesha kupata hospitali ya moyo katika Hospitali ya
Muhimbili. Pamoja na kuwashukuru niliomba idadi iongezwe kwani mahitaji yapo na watu
wanawapenda Madaktari wa China.
Yapo mambo mengi mazuri yaliyofanyika katika
ziara yangu nchini China ambayo tutakesha kama tutahitaji kuyafafanua moja baada ya
jingine. Hata hivyo, napenda kuyazungumzia mambo mawili. Kwanza ni taarifa aliyonipa
Rais Xi Jinping kwamba wanaongeza ufadhili wa masomo kwa kutupa nafasi 100 zaidi kwa
vijana wa Tanzania kusoma China kwa kipindi cha miaka mitano. Pia wamekubali kutusaidia
ujenzi wa chuo cha ufundi (VETA) cha Mkoa wa Kagera. Aidha, wamekubali ombi langu
la kuongeza idadi ya madaktari na wataalamu wa afya kutoka China kuja kufanya kazi
nchini.
Ziara Vietnam Ndugu Wananchi; Baada ya kumaliza ziara
yangu China nilitembelea Vietnam kwa siku mbili. Huko nako nilikwenda kuimarisha na
kuendeleza uhusiano mzuri uliopo kati ya nchi zetu, na kujifunza zaidi kutoka kwa
wenzetu ambao wamepata mafanikio makubwa kiuchumi katika kilimo na viwanda kwa kipindi
kifupi. Hii ni nchi ambayo tulianza nayo mageuzi ya kiuchumi wakati mmoja mwaka 1986.
Wenzetu wameweza kupata mafanikio makubwa katika kilimo, viwanda, ufugaji wa samaki
na mengine mengi. Kwa upande wa teknolojia ya mawasiliano ya simu, wanayo kampuni
ya Viettel ambayo imekuwa kubwa duniani na inakusudia kuwekeza nchini.
Kwa
kweli mafanikio ambayo Vietnam imepata tangu mwaka 1986 yanatupa matumaini kwamba
na sisi Tanzania tunaweza kufanikiwa kama wao. Hatuna budi kujipanga vizuri. Tumekubaliana
kushirikiana zaidi hasa kubadilishana uzoefu na maarifa katika kilimo na viwanda.
Ugonjwa wa Ebola Ndugu Wananchi; Jambo la pili ninalotaka kulizungumzia,
si mara yangu ya kwanza kufanya hivyo. Hili si jingine bali ni tahadhari juu ya maradhi
ya Ebola yaliyoanzia huko Afrika Magharibi katika nchi za Liberia, Sierra Leone na
Guinea. Baadae yalifika Nigeria, Senegal, Mali, Marekani, Spain na Uingereza. Inakadiriwa
kuwa ugonjwa huu hatari umekwishaua watu 4,960 na wengine 13,567 wameambukizwa toka
ulipoanza hadi sasa. Ugonjwa huu umeendelea kuwa tishio la dunia kutokana na kasi
kubwa ya kuenea kwake. Lakini hasa kwamba asilimia 70 mpaka 90 wanaoupata ugonjwa
huu hupoteza maisha. Bahati mbaya hauna dawa wala kinga. Bado wataalamu wa dawa wanachuna
bongo.
Taarifa njema ni kuwa ugonjwa huu haujaingia nchini Tanzania. Hata hivyo,
hii haiondoi ukweli kuwa unaweza kufika kwani watu wanatembea kutoka nchi zenye maradhi
haya na kuja nchini kwetu. Hapa jirani na sisi upo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Sitashangaa pia kwamba wapo Watanzania wanaokwenda nchi zenye maambukizi makubwa hata
wakati huu. Watu hao wana hatari kubwa ya kupata maambukizi.
Narudia kukumbusha
umuhimu wa kuchukua tahadhari kitaifa na kila mtu anayeishi hapa nchini. Sisi Serikalini
tunaendelea kuchukua hatua stahiki na kuimarisha jitihada na hatua za kuwachunguza
wageni katika mipaka yetu ya usafiri wa nchi kavu na usafiri wa anga. Tumejiandaa
vya kutosha kutambua watu wenye joto kubwa zaidi ya joto la kawaida la mwili wa mwanadamu.
Hali kadhalika, tumewataka watu wanaoingia nchini kueleza kama katika wiki
tatu zilizopita wametembelea nchi za Guinea, Sierra Leone na Liberia. Nia ya kutaka
waseme siyo kuwazuia wasiingie nchini bali kuwapa ushauri juu ya dalili za ugonjwa
wa Ebola na nini wafanye iwapo dalili hizo zitawatokea. Pia tunapenda kujua mahala
watakapofikia ili tuweze kuwafuatilia.
Ndugu Wananchi; Ninawaomba ushirikiano
wa kila mmoja wenu kutoa taarifa kwa wakati mara mtakapoona mtu mwenye dalili za ugonjwa
huo ambazo ni homa kali ya ghafla, kutokwa na damu mwilini, kutapika na kuharisha
kwa wakati mmoja. Toeni taarifa ili wataalamu wenye ujuzi na vifaa stahili vya kujikinga
waweze kuja kuwahudumia ipasavyo wagonjwa wenye dalili hizo. Jiepusheni na kumsogelea
au kugusana na mtu wa aina hiyo. Na, maiti aliyekufa kutokana na ugonjwa wenye dalili
hizo pia asiguswe. Kufanya hivyo ni kujiweka kwenye hatari ya moja kwa moja ya kuambukizwa
kwani huenda mtu huyo ni muathirika wa Ebola. Toa taarifa upate maelekezo ya kitaalamu.
Uchaguzi
wa Serikali za Mitaa
Ndugu Wananchi; Kama mnavyofahamu tarehe 14 Desemba,
2014 tutafanya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa ngazi ya vitongoji, mitaa na vijiji.
Tumelazimika kufanya Uchaguzi huo mwezi Desemba, 2014 badala ya mwezi Oktoba kama
ilivyostahili kutokana na shughuli za Bunge Maalum la Katiba kuendelea hadi tarehe
4 Oktoba, 2014 kwa kupitisha Katiba Inayopendekezwa. Kutokana na Taifa kuwa katika
jambo lile kubwa ilionekana ni busara kuacha kwanza mchakato ule ukamilike kabla ya
kufanyika kwa uchaguzi huo.
Nimeambiwa na TAMISEMI kwamba maandalizi ya uchaguzi
huo yanakwenda vizuri na kwamba ratiba imekwishatolewa, na majina ya mitaa, vijiji
na vitongoji vipya nayo yamekwishatolewa. Kazi ya kuandikisha wapiga kura itafanyika
kuanzia tarehe 23 Novemba, 2014 na itamalizika kwa orodha ya wapiga kura kubandikwa
mahali pa wazi hasa kwenye mbao za matangazo katika vitongoji, mitaa, na vijiji husika
ifikapo tarehe 30 Novemba, 2014.
Kufanya hivyo kutawezesha wananchi kukagua
orodha hiyo kuona kama majina yao yapo, na kujiridhisha kuwa majina ya wale walioandikishwa
kwenye daftari hilo ni wapiga kura wenye sifa stahiki za kupiga kura katika uchaguzi
huo katika eneo husika. Nawasihi wananchi wote mjitokeze kwa wingi kujiandikisha na
kukagua orodha ya wapiga kura itakapobandikwa ili kufanikisha zoezi hilo.
Kwa
mujibu wa ratiba ya uchaguzi vyama vya siasa vinapaswa kuwasilisha fomu za wagombea
wao kwa Msimamizi wa Uchaguzi kuanzia tarehe 20 hadi 22 Novemba, 2014. Kwa maana hiyo,
wale wenye shauku, nia na sifa za kugombea uongozi katika uchaguzi ujao wa Serikali
za Mitaa, wanapaswa kutega sikio ili kujua ratiba za uchaguzi na uteuzi ndani ya vyama
vyao ili wapate fursa ya kuteuliwa kugombea.
Napenda kuchukua fursa hii kuwahimiza
wananchi wote wakiwa pia vijana na wanawake wasibakie nyuma, wajitokeze kwa wingi
kugombea nafasi hizo na nyingine katika Uchaguzi Mkuu ujao. Ratiba ya uchaguzi huo
iliyotolewa na TAMISEMI inaonyesha kwamba mikutano ya kampeni ya kuwanadi wagombea
itafanyika kwa siku 14 kuanzia tarehe 30 Novemba, 2014 hadi tarehe 13 Desemba, 2014
siku moja kabla ya siku ya kufanyika kwa uchaguzi huo.
Ndugu Wananchi; Mfumo
wa utawala wa nchi yetu huanzia katika ngazi ya kitongoji na mtaa kisha kijiji, kata
na hatimaye taifa. Kwa hiyo uchaguzi wa vitongoji, mitaa na vijiji ndiyo msingi wa
uongozi na utawala wa nchi yetu. Tukipata viongozi wazuri katika ngazi hii ya msingi,
tutakuwa tumefanikiwa sana katika kuimarisha utawala bora na kuongeza kasi ya maendeleo
yetu. Rai yangu kwenu, wananchi wenzangu ni kuwa mjitokeze kwa wingi wakati wa kampeni
kuwasikiliza wagombea wetu wakijieleza, kisha tuwachague wale watu ambao sisi tunaona
wanatufaa. Lazima tutambue kuwa ngazi ya vitongoji, mitaa na vijiji ndiyo msingi wa
uongozi wa nchi yetu. Tukipata watu wazuri tutakuwa tumejenga msingi imara wa uongozi
katika taifa letu.
Watu wote watakaojitokeza kugombea katika ngazi ya vitongoji,
mitaa na vijiji vyetu ni watu tunaoishi nao na kwamba tunawafahamu vizuri sana. Hatuna
budi kuvitendea haki vijiji, mitaa na vitongoji vyetu kwa kuwachagua viongozi wazuri
watakaokuwa chachu ya maendeleo katika maeneo yetu. Tukifanya makosa ya kuchagua watu
wasiofaa tuelewe kwamba tutakuwa tumejinyima fursa ya kuwa na viongozi bora kwa kipindi
cha miaka 5 ijayo. Pia tunaweza kuzua migogoro na kupunguza kasi ya maendeleo katika
maeneo yetu. Tusione haya kuwashawishi watu wazuri wajitokeze kugombea.
Mchakato
wa Katiba na Kura ya Maoni
Ndugu wananchi, Bunge la Katiba lilikamilisha
kazi yake ya kutunga Katiba mpya ilipofika tarehe 2 Oktoba, 2014 ambayo ilikuwa siku
mbili kabla ya muda uliopangwa wa tarehe 4 Oktoba, 2014. Tarehe 8 Oktoba, 2014, Mwenyekiti
wa Tume ya Katiba aliikabidhi Katiba hiyo kwangu na kwa Rais wa Zanzibar kama yalivyo
matakwa ya Kifungu cha 28A(1) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. Kwa mara nyingine
tena nawapongeza kwa dhati aliyekuwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel
John Sitta, Makamu wake Mhe. Samia Suluhu na Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba kwa
kazi kubwa na nzuri. Wametupatia Katiba Inayopendekezwa inayojitosheleza kwa kila
hali. Nawapongeza pia Makatibu wa Bunge, Sekretarieti yao na wafanya kazi wote. Bunge
Maalum la Katiba linastahili pongezi nyingi kwa kazi nzuri waliyofanya na hasa kwa
kuikamilisha ndani ya muda wa uliopangwa wa siku 130 tu. Baadhi ya nchi duniani jukumu
hili limechukua muda mrefu zaidi ya uliokusudiwa au hata kushindikana.
Tutakuwa
wachoyo wa fadhila tusipoipongeza Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya uongozi wa
Mwenyekiti Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba na Makamu wake Mheshimiwa Jaji Augustino
Ramadhani pamoja na Wajumbe wote wa Tume hiyo. Tunawapongeza kwa kutayarisha Rasimu
nzuri ya Katiba ambayo ndiyo iliyoliongoza Bunge Maalum la Katiba kupata Katiba Inayopendekezwa
iliyo bora. Kilichobakia ni kuwaachia wananchi kuamua kama wanaitaka Katiba Inayopendekezwa
au hapana. Watafanya hivyo kwenye kura ya maoni itakayofanyika kwa mujibu wa Sheria
ya Mabadiliko ya Katiba na Sheria ya Kura ya Maoni iliyotungwa kutekeleza matakwa
ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.
Ndugu wananchi, Miaka ya nyuma kulikuwa
na tangazo la sabuni ya Omo lililokuwa likisema “Uzuri wa Ngoma Sharti Uicheze”. Uzuri
wa Katiba Inayopendekezwa siyo wa kuambiwa. Unahitaji uione, uisome na uielewe. Imeandikwa
kwa Kiswahili rahisi na fasaha. Inasomeka na kueleweka kwa urahisi sana. Ni rai yangu
kwamba wananchi wote muipate nakala ya Katiba Inayopendekezwa na mjisomee. Sheria
imeniagiza kuichapisha Katiba hiyo kwenye gazeti la Serikali ndani ya siku saba baada
ya kukabidhiwa. Nimekwisha kufanya hivyo. Aidha, Sheria inaeleza kwamba Katiba Inayopendekezwa
isambazwe kwenye magazeti ya kawaida ndani ya siku 14. Zoezi hili ni endelevu. Usambazaji
wa Katiba Inayopendekezwa unaendelea na utaendelea mpaka Kura ya Maoni itakapopigwa.
Wito wangu kwenu Watanzania wenzangu ni kwamba msikubali kulaghaiwa na maneno
ya wale wachache wanaotaka kuturudisha nyuma na kutunyima fursa ya kupata Katiba iliyo
bora zaidi. Maana hapajawahi kutokea ushiriki mpana kama huu katika kutengeneza Katiba
katika nchi yetu. Pengine, hata kwingineko duniani si wengi wametoa fursa kama tulivyofanya
sisi.
Kura ya Maoni Ndugu wananchi, Sheria ya Kura ya Maoni iliniagiza
kutangaza tarehe ya Kura ya Maoni katika Gazeti la Serikali ndani ya siku 14 baada
ya kupokea Katiba Inayopendekezwa. Nimefanya hivyo. Awali Sheria hiyo iliagiza Kura
ya Maoni ifanyike na matokeo yake yajulikane ndani ya siku 70. Waziri mwenye dhamana
ya Uchaguzi alipowauliza viongozi wa Tume ya Uchaguzi kuhusu utekelezaji wa matakwa
hayo ya Sheria, Tume ilisema isingweza kuendesha Kura ya Maoni ndani ya muda huo.
Mambo yanayohitajika ni mengi mno ambayo hayawezi kukamilika katika muda huo. Wakaomba
wapewe muda zaidi. Bahati nzuri Kifungu 51 cha Sheria ya Kura ya Maoni kimetoa mamlaka
kwa Waziri mwenye dhamana ya Uchaguzi baada ya kushauriana na Waziri anayehusika na
Uchaguzi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kubadilisha masharti haya kama kutakuwa
na umuhimu wa kufanya hivyo.
Baada ya mashauriano hayo, Mawaziri wenye dhamana
ya uchaguzi wa pande zetu mbili za Muungano waliridhika kuwa upo umuhimu wa kusogeza
mbele muda ili kutoa fursa kwa Tume kukamilisha taratibu inazowajibika kufanya. Hayo
ni pamoja na kuboresha Daftari la Kudumu la Mpiga Kura, matayarisho ya upigaji wa
Kura ya Maoni na mambo mengine kadhaa.
Hivyo basi, tarehe 03 Oktoba, 2014,
Waziri mwenye dhamana ambaye ni Waziri Mkuu kwa kutumia mamlaka aliyopewa ya Kifungu
cha 51 cha Sheria ya Kura ya Maoni, alitangaza kupitia gazeti la Serikali kubadilisha
sharti la siku 70 na kuacha Rais aamue siku ya kupiga kura. Kwa sababu ya mabadilikio
hayo, tarehe 10 Oktoba, 2014 nilitangaza kupitia Gazeti la Serikali kuwa Kura ya Maoni
itakuwa tarehe 30 Aprili, 2015 ili kutoa fursa kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kukamilisha
taratibu zake. Katika tangazo hilo pia, nilielekeza kuwa kampeni zitaanza tarehe 30
Machi na kuisha tarehe 29 Aprili, 2014 siku moja kabla ya siku ya kupiga kura, kama
ilivyo desturi yetu katika upigaji kura hapa nchini.
Ndugu Wananchi; Natambua
kuwepo dhana kuwa siku za kampeni ni 60. La hasha! Siku za Kampeni zinaamuliwa na
Rais, kufuatia Kifungu cha 4 (2) b kisemacho: “Amri kwa ajili ya kura ya maoni itakuwa
kama ilivyo kwenye fomu iliyotajwa kwenye jedwali la Sheria hii, na itaainisha: (a)
Katiba Inayopendekezwa kuandikwa; (b) Kipindi ambacho kampeni kwa ajili ya Kura
ya Maoni itafanyika; (c) Kipindi ambacho Kura ya Maoni itafanyika”
Tume
ya Uchaguzi ina mamlaka ya kuruhusu vyama vya kijamii na vya kiraia kutoa elimu ya
umma ndani ya siku 60 kabla ya siku ya Kura ya Maoni. Tume imepewa mamlaka hayo na
Kifungu cha 5 (4) cha Sheria ya Kura ya Maoni. Kwa sababu hiyo, nawaomba Watanzania
wenzangu tuzingatie matakwa ya Sheria ya Maoni ambayo imeelekeza vizuri kuhusu lini
Kura ya Maoni itafanyika na lini wadau watoe elimu kwa umma. Naomba tuwe na subira
mpaka hapo Tume ya Uchaguzi itakapotoa maelekezo ya utekelezaji wa fursa husika kwa
wadau.
Ndugu wananchi, Ni matarajio yangu kwamba wananchi wote mtajitokeza
kwa wingi kwenda kuboresha taarifa zenu kwenye Daftari la Kudumu la Mpiga Kura kama
itakavyoelekezwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi, na hatimaye itakapofika tarehe 30 Aprili,
2015 mtakwenda kwa wingi kupiga kura ya kuamua kuhusu hatma ya Katiba Inayopendekezwa.
Naomba mfanye uamuzi mzuri. Fursa hii ni adhimu na ya kihistoria ambayo tukiipoteza
huenda itachukua miaka mingi kuipata tena. Mtakapokuwa mnakwenda kupiga kura zingatieni
maslahi yenu pamoja na ya watoto na wajukuu zenu, maana Katiba ndiyo inayoweka misingi
na mstakabali wa taifa letu sasa na karne nyingine zijazo.
Hitimisho Ndugu
Watanzania wenzangu, Naomba nimalizie kwa kuwasihi mjitokeze kwa wingi kushiriki
katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika tarehe 14 Desemba, 2014. Endeleeni
kusoma Katiba Inayopendekezwa ili muda utakapofika kila mtu atoe uamuzi stahiki na
wenye maslahi kwa nchi yetu. Nimezitaka Wizara na Taasisi zinazohusika na utekelezaji
wa makubaliano yetu na Serikali ya China na Vietnam kuchukua hatua za ufuataliaji
na wanipe taarifa. Narudia kutoa wito tuendelee kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa
wa Ebola. Nawaomba muendelee kuiunga mkono Serikali yetu katika jitihada zake za kuiletea
maendeleo nchi yetu na watu wake.
Mwisho, ingawa siyo kwa umuhimu, vijana
wetu 297,488 wameanza mtihani wa taifa wa kidato cha nne jana tarehe 3 Novemba, 2014.
Tuna imani wamejiandaa vya kutosha na wameandaliwa vyema na walimu, wazazi na walezi
wao kwa ajili ya mtihani huo. Naungana na walimu, wazazi, walezi na Watanzania wote
kuwatakia kila la heri katika mtihani wao huo.
Mungu Ibariki Afrika! Mungu
Ibariki Tanzania! Ahsanteni Sana kwa kunisikiliza!