2014-11-04 09:14:56

Novena kwa ajili ya kuombea haki, amani na upatanisho Burkina Faso


Kardinali Philippe Nakellentuba Ouèdraogo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Ouagadougou, Burkina Faso, anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema nchini Burkina Faso kuungana kwa pamoja ili kusali kwa ajili ya kuombea haki, amani na utulivu katika kipindi hiki kigumu cha historia ya nchi yao, baada ya nguvu ya umma kumlazimisha Rais Blaise Compaorè, tarehe 30 Oktoba 2014 kutema ngazi na kukimbilia uhamishoni Pwani ya Pembe, baada ya jitihada za kutaka kubadili Katiba ya nchi kushindikana.

Kwa sasa Serikali ya mpito inaongozwa na Jeshi, chini ya Luteni Kanali Isaac Zida, moja ya askari kikosi cha ulinzi wa Rais. Serikali ya mpito inasema, itarudia utawala wa kiraia mapema iwezekanavyo, lakini vyama vya upinzani vinataka utawala wa kiraia kuongoza nchi na wala si kuendekeza tena masuala ya mapinduzi ya kijeshi ambayo yameligharimu sana Bara la Afrika!

Waamini nchini Burkina Faso tangu tarehe 2 hadi tarehe 9 Novemba 2014 wanasali kwa ajili ya kuombea upatanisho wa kitaifa, haki na amani nchini Burkina Faso. Kardinali ametunga sala maalum akimwomba Mwenyezi Mungu awasaidie watunga sheria hekima na busara itakayohakikisha ustawi na maendeleo; uhuru, haki na amani kwa wananchi wote wa Burkina Faso.







All the contents on this site are copyrighted ©.