Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la Familia anasema, umefika
wakati kwa familia kutoka kifua mbele, ili kushuhudia dhamana na utume wake katika
maisha ya hadhara. Kanisa linabeba dhamana na wajibu mkubwa wa kuwaonesha walimwengu
uhusiano uliopo kati ya Bwana na Bibi katika kuendeleza uzao wa binadamu. Muungano
huu ni msingi thabiti katika ujenzi wa Jamii ya binadamu na mahusiano yake.
Askofu
mkuu Paglia ameyasema haya wakati wa uzinduzi wa Kongamano la Kumi na Sita la Wakatoliki
na Maisha ya Hadhara, lililoandaliwa na Vyama vya Kitume vya Kikatoliki kwa kushirikiana
na Mfuko wa Chuo Kikuu cha San Pablo, utakaofanyika Jimbo kuu la Madrid, kuanzia tarehe
14 hadi tarehe 16 Novemba 2014, huku wakiongozwa na kauli mbiu "Familia: changamoto
na matumaini".
Jambo msingi anasema Askofu mkuu Paglia kwamba, familia inadhamana
ya kuendeleza zawadi ya maisha inayofumbatwa katika Fumbo la upendo kati ya Bwana
na Bibi. Hii ni dhamana inayotekelezwa na Familia imara na thabiti na hata zile ambazo
zinamadonda na majeraha makubwa katika maisha na utume wao. Hii ni changamoto kwa
familia kuhakikisha kwamba, zinajitokeza katika maisha ya hadhara ili kushuhudia utume
na dhamana yake katika Jamii, kwa kushirikisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia
kama kielelezo cha imani tendaji.
Familia za Kikristo hazina budi kuonesha
mshikamano wa dhati na Kanisa, kwani Kanisa ni mlinzi na mtetezi mkuu wa tunu msingi
za maisha ya ndoa na familia ambazo zinapigwa danadana katika ulimwengu mamboleo.
Mahusiano kati ya Familia na Kanisa bado hayajapata nguvu sana, mwaliko kwa wanandoa
kuimarisha zaidi mahusiano haya, ili kwa pamoja kukabiliana na changamoto zinazojitokeza
katika maisha ya ndoa na familia.