Wapendwa taifa la Mungu, Kanisa linawaombea marehemu ili watakaswe, ikiwa wanahitaji
kutakaswa kabla ya kupokelewa mbinguni wakati miili yao inapobaki ardhini ikingoja
kurudi kwa Kristo na ufufuko wa wafu. Hii ndiyo sababu Kanisa linatolea sadaka ya
misa kwa ajili ya marehemu. Mtakatifu Monika, mama yake Mtakatifu Agustino, anaongezea
thamani kuhusu ufuhamu huu. Alipokuwa katika hatari ya kufa, aliwaomba watoto wake
na kusema, “ mnaweza kunizika popote mnapotaka lakini msinisahau katika Altare ya
Bwana.”
Kanisa linasali na kuwaombea marehemu kusudi wapate msaada wa kiroho
na waamini walio bado hai wapate matumaini ya uzima ujao mbinguni. Ni muhimu na vema
kuwaombea wafu, kwani hata kama wamekufa katika neema na upendo kwa Mungu, inawezekana
bado wanahitaji utakaso wa mwisho ili waweze kuingia katika furaha ya mbingu.
Mtakatifu
Ireneo anatupatia tafakari hii nzuri sana – utukufu wa Mungu ni mwanadamu aliye hai.
Maisha ya mwanadamu, mkristo, mbatizwa huwa na aina mbili ya kifo. Kifo cha kwanza
ni kwa njia ya ubatizo na imani – Rum. 1,6 – ambao katika hao ninyi mmekuwa wateule
wa Yesu Kristo - tumejiunga na Kristo aliyekufa na kufufuka. Katekisimu Mpya ya Kanisa
Katoliki namba: 628 inasema ubatizo ambao alama yake ya asili na timilifu ni kuzamishwa,
waashiria bayana kushuka kaburini kwa mkristo - anayeifia dhambi pamoja na Kristo
ili aishi maisha mapya.
Tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti
yake, kusudi kama Kristo alivyofufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa Baba, vivyo
hivyo na sisi tuenende katika upya wa uzima – Rom. 6,4; Kol. 2,12 – mkazikwa pamoja
naye katika ubatizo, na katika huo mkafufuliwa pamoja naye, kwa kuziamini nguvu za
Mungu aliyemfufua katika wafu; Efe. 5,26.
Aina ya pili ya mauti aipatayo mkristo
huwa sawa na ile impatayo mwanadamu ye yote, yaani ni wakati utokeapo utengano wa
mwili na roho hapa duniani. Kama tunavyoshudia leo tunapoona kuwa ndugu yetu hayupo
nasi tena kimwili. Ndugu zangu – KKK 990 – neno mwili laeleza mtu katika hali yake
ya udhaifu na ya kufa – Mwa. 6,3; Zab. 56,5; Isa. 40,6.
Hivi mwanadamu aliye
katika hali ya mwili na aliye na mwanzo hufika kikomo. Hufikwa na mauti. Ila katika
kitabu cha Hek. 1,13 – tunasoma kuwa, Mungu hakuifanyiza mauti, wala haimpendezi walio
hai wakipotea; Rom. 5,12. Ila katika KKK 1008 na 413 tunaona kuwa; kifo ni tokeo
la dhambi. Na kwamba mwanadamu ndiye asili ya mauti – kinyume cha muumba wake – Mwa.
3. Kifo cha kweli ni kifo cha mwenye dhambi.
Mamlaka ya ufundishaji wa Kanisa,
mfafanuzi halisi wa matamshi ya Maandiko Matakatifu na mapokeo hufundisha kwamba kifo
kimeingia ulimwenguni kwa sababu ya dhambi ya mwanadamu –Ingawa mwanadamu ana hali
ya kufa, Mungu alimweka asife. Kifo kilikuwa ni kinyume cha mipango ya Mungu Muumbaji,
nacho kiliingia ulimwenguni kama tokeo la dhambi – Hek. 2,23-24. Kifo cha kimwili,
ambacho mwanadamu angekuwa huru nacho, ndiye adui wa mwisho wa mwanadamu ambaye lazima
kumshinda – 1Kor. 15,26 – adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti.
Mbele
ya kifo fumbo la hali ya kibinadamu linakuwa kubwa sana - KKK 1006. Kwa namna moja
kifo cha mwili ni kawaida, lakini kwa imani kwa kweli kifo ni mshahara wa dhambi –
Rom. 6,23; - kwa maana mshahara wa dhambi ni mauti, bali karama ya Mungu ni uzima
wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu. Na katika Mwa. 2,17 tunasoma haya – walakini
matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda
ya mti huo utakufa hakika.
Lakini sisi tunamshukuru Kristo aliyetupatia matumaini
mapya. Kwa wale wanaokufa katika neema ya Kristo, kifo ni ushirika katika kifo cha
Bwana, ili kuwezza kushiriki pia ufufuko wake. Tuna uhakika kuwa kwa njia ya Kristo
– tunapata uzima mpya – Rum. 8,29, - maana wale aliowajia tangu asili, aliwachagua
tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni
mwa ndugu. 2Kor. 5,17, - hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya,
ya kale yamepita, tazama, yamekuwa mapya. Yoh. 14, 5-6 – Tomaso akamwambia, Bwana,
sisi hatujui uendako, nasi twaijuaje njia? Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia na kweli
na uzima, mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. Yoh. 3,5 – Yesu akajibu, amini,
amini, nakuambia, mtu asipozaliwa kwa maji na Roho, hawezi kuuingia ufalme wa Mungu.
Mk. 16,16 – aaminiye na kubatizwa ataokoka, asiyeamini atahukumiwa.
Mtume
Paulo anaelezea mauti na aina fulani ya ukombozi – Rum. 7,1…. Kwa kifo cha huyo mtu
– tunakombolewa na maisha ya zamani – Rum. 7,1-5. – kwa maana tulipokuwa katika hali
ya mwili, tamaa za dhambi, zilizokuwako kwa sababu ya torati, zilitenda kazi katika
viungo vyetu hata tukaizalia mauti mazao. Bali sasa tumefunguliwa katika torati, tumeifia
hali ile iliyotupinga, ili sisi tupate kutumika katika hali mpya ya roho, si katika
hali ya zamani, ya andiko
Mtume Paulo akiongea juu ya kifo chake anasema -
2Tim 4:7-8 “Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, imani nimeilinda;
baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa
siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake.” Mtume
Paulo aliwekeza katika Kristo na matumaini yake ni kuupata uzima wa milele. Tena ana
hakika ya hilo. Anatualika nasi tuwekeze katika Bwana.
Pengine swali ambalo
mwanadamu asumbuka nalo baada ya Fumbo la kifo ni hili: Wafu wanafufuka namna gani?
KKK 997 – kufufuka maana yake nini? Wafufuliwaje wafu? Nao huja kwa mwili
gani? Ewe mpumbavu, uipandayo haikui isipokufa, nayo uipandayo hupandi mwili ule utakaokua
ila chembe tupu … hupandwa katika uharibifu, hufufuliwa katika kutoharibika; wafu
watafufuliwa wasiwe na uharibifu…maana sharti huu uharibikao, uvae kutoharibika, nao
huu wa kufa uvae kutokufa – 1Kor. 15,35-53.
Kwa kifo, utengano wa roho
na mwili, mwili wa mtu huoza, pindi roho yake huenda kukutana na Mungu ikingojea kuunganika
na mwili uliotukuka. Mungu, kwa uwezo wake mkuu, atairudishia kwa hakika miili yetu,
uzima usioharibika kwa kuiunganisha na roho zetu, kwa nguvu ya ufufuko wa Yesu.
Siri
iliyo kuu na ngumu - KKK – 1005 – ili kufufuka pamoja na Kristo, ni lazima kufa pamoja
na Kristo; ni lazima kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana – 2Kor. 5,8
– lakini tunao moyo mkuu, nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa
pamoja na Bwana. Katika kwenda huko, yaani kifo, roho hutengana na mwili – Fil. 1,23.
Nayo itaungana na mwili wake siku ya ufufuko wa wafu. . – Rum. 8,11 – lakini, ikiwa
Roho wake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo
Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho wake
anayekaa ndani yenu. Ili tufufuke ni lazima kufa pamoja na Kristo. Hapa ndipo mwanadamu
anapata mahangaiko. Tunapata shida sana kupokea hili. Tunatamani uzima wa milele lakini
kifo kinatusumbua mno.
Na zaidi sana katika wasiwasi huo mwanadamu huendelea
kujiuliza -– nani atafufuka? KKK – 998 - Watu wote waliokufa. Wale waliofanya mema
kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu - Yoh. 5,29; Dan.
12,2 –tena, wengi wa hao walalao katika mavumbi ya nchi wataamka, wengine wapate uzima
wa milele, wengine aibu na kudharauliwa milele .
Na tena – namna gani? KKK
999 – kwa namna ya Kristo. Kristo amefufuka pamoja na mwili wake hasa – tazameni
mikono yangu na miguu yangu ya kuwa ni Mimi mwenyewe. – Lk. 24,39, lakini hakuurudia
uzima wa kidunia. Wakati huo huo walio wake Kristo watafufuka pamoja na miili yao
wenyewe waliyo nayo sasa, lakini mwili huo utageuzwa katika mwili mtukufu, katika
mwili wa kiroho – Fil. 3,21; 1Kor. 15,44.
Ni msalaba wa Kristo pekee unaoweza
kutupa majibu na sababu za hayo mateso tunayoyashuhudia kutokana na kifo. Lakini pia
msalaba hutoa majibu kwa fumbo ambapo kwa sasa ni vigumu kulielewa kwani lipo juu
ya uelewa wetu. Kwa hiyo tuna uhakika kuwa kifo cha Kristo ndilo jibu ambalo Mungu
analitoa katika nyakati zote mbili za furaha na uchungu.
Ufufuko wa mwili
huonyesha kwamba baada ya kifo hakutakuwa na uzima wa roho peke yake bali kwamba hata
miili yetu yenye hali ya kufa itapata tena uzima – Rom. 8,11 – lakini, ikiwa Roho
wake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo
Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho wake
anayekaa ndani yenu.
Mwadilifu, maana yake asiye na dhambi, afungamanaye na
Mungu, hafi kabisa – Hek, 11,26 – lakini wewe unaviachilia vyote, kwa kuwa ni vyako,
Ee Mfalme Mkuu mpenda roho za watu, maana roho yako isiyoharibika imo katika vyote.
Mungu aliye hai ametuumba sisi ili tuwe hai. Hivyo kifo si mwisho wa maisha
yetu. Mwisho wa maisha yetu hapa duniani ni mwanzo wa maisha mapya na Mungu. Ndivyo
inavyotufundisha imani yetu. Kifo hakina sauti ya mwisho. Ushindi wa Msalaba ndiyo
matumaini yetu. Kristo ameshinda dhambi na mauti. Ndiyo matumaini yetu. Nasi tunaalikwa
kuwekeza katika matumaini hayo.
Matumaini yetu ni uhai, tena ule wa kimungu.
Tuongozwe na matumaini haya. Tutafakari tena na Mt. Ireneo – UTUKUFU WA MUNGU NI
MWANADAMU ALIYE HAI.