2014-11-03 07:55:27

Maana ya Sala ya Kikristo!


Bwana, tufundishe kusali, Lk. 11:1-4. Ni kauli iliyotolewa na Mitume wa Yesu baada ya kumwona akisali kwa umakini mkubwa, kiasi cha kuacha mvuto na chapa katika hija ya maisha yao ya kiroho. RealAudioMP3

Wataalam wa masuala ya maisha ya kiroho wanabainisha kwamba, mtu anayefahamu kusali vyema, ana uwezo wa kuwafundisha wengine kusali vizuri zaidi, kwani ni mtu aliyefundwa, akafundika katika kujenga na kuimarisha mahusiano na Mwenyezi Mungu pamoja na jirani zake. Hivi ndivyo ilivyokuwa kwa Yohane Mbatizaji, lakini zaidi kwa Yesu Mwenyewe!

Mtu wa sala au mchamungu anatambua fika kwamba, sala ni nguzo ya maisha inayomwezesha mwamini kujenga mahusiano thabiti na Mwenyezi Mungu pamoja na jirani zake. Huu ni utambuzi kwamba, daima Mwenyezi Mungu yuko tayari kusikiliza sauti na kilio cha waja wake, wakati wote wanapomkimbilia kwa imani na matumaini. Huu ndio urithi mkubwa ambao Yesu Kristo amewaachia wafuasi wake katika hija ya maisha yao ya kiroho, baada ya kumwona anasali kwa umakini mkubwa, tofauti kabisa na walimu wengine waliokuwepo nyakati hizo.

Sala makini inahitaji maandalizi ya dhati, kwani sala ni sanaa; ni sayansi, ni utambuzi, lakini zaidi ya yote ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwa ajili ya wengine. Sala ni nguvu ya ndani na wala si wingi wa maneno. Ni mwelekeo wa kutambua kwamba, Mwenyezi Mungu ni Baba mwema, mwingi wa huruma na mapendo. Kwa mwamini anayependa kusali kwa dhati kabisa anapaswa kuwa na imani thabiti sanjari na kuonesha utii, ili kuimarisha mahusiano yake na Mungu pamoja na jirani zake, walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.