2014-11-01 14:23:28

Katiba mpya itawasaidia kuchuchumilia utakatifu wa maisha!


Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kimissionari na Kazi za Kitume, limepitisha Katiba ya Shirika la Wafuasi wa Yesu, hapo tarehe 16 Oktoba 2014. Shirika linapenda kuchukua fursa hii kuwapongeza kwa namna ya pekee Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI, Papa Francisko, Kardinali Velasio De Paolis na washauri wake walioliwezesha Shirika kufikia hatua hii baada ya kupitia katika kipindi cha giza na hali tete katika maisha na utume wake.

Katiba Mpya ya Shirika inafumbata kanuni msingi zinazopania kulinda na kudumisha karama ya Shirika pamoja na kuiendeleza. Hayo yamebainishwa na Padre Eduardo Robles-Gil, Mkuu wa Shirika la Wafuasi wa Yesu. Katiba hii inatekeleza kwa dhati mambo msingi ambayo yalibainishwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI katika mchakato wa kulipyaisha Shirika, ulioanza kunako mwaka 2010 kwa kumteua Kardinali Velasio De Paolis kuwa msimamzi wa kipapa, dhamana iliyoendelezwa na Baba Mtakatifu Francisko alipoingia madarakani.

Katiba mpya ni matunda ya kazi ya miaka mitatu iliyofanywa kwa njia ya sala na tafakari ya kina, kwa kuwashirikisha wanashirika wote katika hatua mbali mbali na hatimaye, kuitishwa kwa mkutano mkuu wa Shirika uliohitimisha rasmi dhamana ya Kardinali De Paolis, mkutano ambao uliadhimishwa kati ya Mwezi Januari na Februari 2014.

Katiba hii inalenga kuwasaidia anasema Padre Eduardo Robles-Gil wanashirika kuchuchumilia utakatifu wa maisha sanjari na kutekeleza utume wao ndani ya Kanisa, kwa kuwahudumia Watu wa Mungu, mintarafu maisha ya kitawa miongoni mwa Wafuasi wa Yesu.







All the contents on this site are copyrighted ©.