2014-10-29 08:38:18

Zambia inaomboleza kifo cha Rais Sata "King Cobra"


Rais Michael Sata wa Zambia aliyekuwa na umri wa miaka 77 amefariki dunia Jumanne tarehe 28 Oktoba 2014 mjini London, alikokuwa amelazwa kwenye Hospitali ya Mfalme Edward VII. Marehemu Rais Sata aliondoka Zambia tarehe 19 Oktoba 2014 kuelekea London kwa matibabu, huku akiwa amesindikizwa na familia yake.

Minong'ono kwamba, Rais Sata alikuwa anaumwa sana ilianza kusikika kunako mwezi Juni, alipoweka hadharani na kuelekea Israeli kupata matibabu. Mwezi Septemba alipangiwa kuhutubia kwenye Baraza kuu la Umoja wa Mataifa, lakini alishindwa kufanya hivyo kutokana na sababu za kiafya na tangu wakati huo hakuweza kuonekana tena hadharani miongoni mwa wananchi wake.

Rais Sata amefariki dunia wakati Zambia bado inasherehekea Jubilee ya miaka 50 tangu ilipojipatia uhuru wake kutoka kwa Mwingereza. Zambia inatarajia kufanya uchaguzi mkuu katika kipindi cha siku 90 kuanzia sasa.

Marehemu Rais Michael alizaliwa tarehe 6 Julai 1973 huko Mpika, Zambia. Baada ya kugombea urais kwa mara tano, hatimaye tarehe 23 Septemba 2011 akachaguliwa kuwaongoza wananchi wa Zambia. Alifahamika na wengi kwa jina la utani "King Cobra", atakumbukwa na wengi kwa mikakati ya maendeleo endelevu kwa wananchi wa Zambia. Waziri wa ulinzi Bwana Edgar Lungu anatarajiwa kuiongoza Serikali ya Zambia katika kipindi hiki cha mpito kuelekea uchaguzi mkuu.







All the contents on this site are copyrighted ©.