Rais Evo Morales akutana na Papa Francisko mjini Vatican
Baba Mtakatifu Francisko, Jumanne tarehe 28 Oktoba 2014 amekutana na kuzungumza na
Rais Evo Morales wa Bolivia mjini Vatican. Rais Morales anashiriki katika mkutano
wa wanaharakati kutoka sehemu mbali mbali za dunia, mkutano ambao umeandaliwa na Baraza
la Kipapa la haki na amani.
Hayo yamebainishwa na Padre Federico Lombardi
msemaji mkuu wa Vatican wakati alipokuwa anajibu maswali ya waandishi wa habari mjini
Vatican siku ya Jumanne. Ziara ya Rais Morales kwa Baba Mtakatifu ni binafsi kwani
haikufuata protokali za kidiplomasia.
Padre Lombardi anasema, Baba Mtakatifu
Francisko amependa kumwonesha mshikamano wake wa kidugu katika mchakato wa kusimama
kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu. Hizi ni dalili njema za maboresho
ya mahusiano kati ya Serikali na Kanisa nchini Bolivia.
Baba Mtakatifu Francisko,
Jumanne asubuhi, alipata fursa ya kuzungumza na wanahakari wa kutetea utu na heshima
na binadamu kwa kukazia kwamba, umilikaji wa ardhi, makazi bora na fursa za ajira,
utu na heshima ya binadamu ni mambo msingi katika Mafundisho Jamii ya Kanisa yanayopata
chimbuko lake kutoka katika Maandiko Matakatifu. Kusimamia haki hizi msingi si kielelezo
cha kuwa ni Mkomunisti!