2014-10-28 07:45:46

Amani na utulivu ni vichocheo vya maendeleo endelevu!


Kwa mara ya kwanza Rais Yoweri Kaguta Museveni alitembelea na kuzungumza na waandishi wa habari wa Radio Vatican kunako mwaka 2001 na tarehe 27 Oktoba 2014 mara baada ya kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko mjini Vatican alitembelea tena Radio Vatican na kuzungumzia kwa namna ya pekee mchango wa dini katika ustawi na maendeleo ya wananchi wa Uganda; uwekezaji, amani na usalama; usalama wa chakula Uganda pamoja na maandalizi ya uchaguzi mkuu, unaotarajiwa kufanyika nchini Uganda kunako mwaka 2015.

Rais Museveni anasema, kimsingi Waganda kama walivyo watu wengi Barani Afrika walikuwa na imani zao za jadi, lakini ujio wa Wakristo na Waislam, ulileta mwelekeo mpya kuhusiana na uelewa wa Mwenyezi Mungu kama Muumbaji na maisha baada ya kifo. Dini zimechangia kwa kiasi kikubwa dhana ya msamaha na upatanisho badala ya kulipizana kisasi pamoja na mapendo kwa Mungu na jirani; tunu msingi katika maisha ya kiroho kwa kila mwamini. Serikali ya Uganda inaheshimu uhuru wa kuabudu.

Rais Museveni anasema kwamba, Kanisa Katoliki limechangia kwa kiasi kikubwa katika ustawi na maendeleo ya wananchi wa Uganda katika sekta ya elimu, afya, maji na maendeleo endelevu, kiasi kwamba, wananchi wa Uganda wanaendelea kucharuka katika maboresho ya maisha yao ya kila siku.

Serikali ya Uganda inaendelea kuwaalika wawekezaji kutoka ndani na nje ya Uganda ili kuwekeza katika sekta ya miundo mbinu, nishati, usafiri, kilimo, ufugaji na uvuvi wa kisasa, bila kusahau utalii na uzalishaji wa bidhaa viwandani. Uganda itaendelea kuweka mazingira bora kwa wawekezaji na kwamba, hakuna anayebaguliwa, bali jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, kila mwekezaji awe ni wa ndani au wa nje anafuata sheria na kanuni msingi zilizowekwa.

Rais Museveni anasema, Uganda itaendelea kusaidia mchakato wa upatikanaji wa amani na utulivu katika nchi za Afrika Mashariki, kwa kushiriki katika mikakati ya ulinzi na usalama. Lengo ni kuhakikisha kwamba, amani inapatikana kwa wote na kwamba hiki ni kichocheo kikubwa cha ustawi na maendeleo ya watu wa Bara la Afrika.

Rais Museveni akizungumzia kuhusu mikakati ya kuwa na uhakika wa usalama wa chakula nchini Uganda anasema, kimsingi Uganda imebahatika kuwa na ardhi yenye rutuba nzuri na vyanzo vingi vya maji na kwamba, kwa miaka mingi Waganda wamejielekeza katika sekta ya kilimo na kwamba, Uganda ina chakula cha kutosha. Jambo la msingi ni wananchi kujifunza sasa kula lishe bora kwa ajili ya afya zao. Uhakika wa usalama wa chakula unachangiwa na uwezo wa watu kununua chakula kilichopo sokoni. Wananchi wa Uganda wana uwezo wa kujinunulia chakula kwa wakati huu.

Rais Museveni katika mahojiano na Radio Vatican anabainisha kwamba, kwa sasa Serikali yake inaendelea kujiandaa kwa ajili ya mchakato wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika hapo mwakani kwa: kujikita katika utoaji wa huduma bora; kwa kuwekeza katika miundo mbinu; amani na utulivu pamoja na kujitegemea. Anasema Serikali yake inapenda kutambulikwa kwa vitendo na wala si kwa maneno matupu na kwamba, uchaguzi mkuu ni majumuisho ya mikakati yote hii inayopania ustawi na maendeleo ya wananchi wa Uganda.

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.







All the contents on this site are copyrighted ©.