2014-10-27 09:37:42

Zawadi ya maisha, utu na heshima ya binadamu ni mambo msingi katika kukuza amani!


Kongamano la Kimataifa la siku mbili lililoandaliwa na Mfuko wa Josefu Ratzinger na kuhudhuriwa na washiriki zaidi ya elfu moja kwenye Chuo Kikuu cha Kipapa cha Medellin, nchini Colombia, kwa kuongozwa na kauli mbiu, “heshima kwa zawadi ya maisha ni njia ya amani” lilipata baraka ya ujumbe kutoka kwa viongozi wakuu wa Kanisa Katoliki.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, amewataka washiriki wa kongamano hili la kimataifa kuzingatia kwa makini Mafundisho ya Kanisa yanayokazia umuhimu wa kulinda, kutunza na kudumisha zawadi ya maisha, kama kiungo muhimu sana cha amani duniani. Hii ni dhamana inayopaswa kumwilishwa katika mioyo ya waamini na watu wote wenye mapenzi mema.

Baba Mtakatifu anasema, utandawazi unaufanya ulimwengu kuwa kama kijiji, lakini kwa bahati mbaya watu hawawezi kuishi kwa umoja na mshikamano kama ndugu na matokeo yake, kinzani na migogoro ya kijamii inazidi kushamiri siku hadi siku. Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kujenga na kudumisha utamaduni wa watu kukutana, kuchuchumilia mafao ya wengi sanjari na kuheshimu utu wa binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu; mambo msingi katika mchakato wa maendeleo endelevu na mshikamano na wote.

Papa Mstaafu Benedikto XVI katika ujumbe wake kwa washiriki wa kongamano hili la kimataifa anasema kwamba, ni tukio ambalo limejitahidi kusoma alama za nyakati kwa kuangalia matatizo na changamoto zinazowakabili walimwengu kwa sasa. Kutafuta, kulinda na kudumisha amani ni changamoto endelevu kwa nyakati hizi kutokana na ukweli kwamba, kuna maeneo mengi ya dunia ambamo vita inazidi kusababisha vifo na majanga mbali mbali.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI anasema, imani kwa Mwenyezi Mungu, Muumba wa vyote ni msingi unaomsukuma mwanadamu kulinda na kutetea maisha, utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Hii ni haki yake msingi. Amani na utu wa mwanadamu ni mambo ambayo yanapata msingi wake katika imani kwa Mwenyezi Mungu.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI amekumbusha kwamba, mara baada ya maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, Mababa wa Kanisa kutoka katika Nchi za Amerika ya Kusini, walikusanyika kwa mara ya kwanza huko Medellin; mkutano ambao ulizinduliwa na Mwenyeheri Paulo VI aliyewatakia amani ya kweli inayopata chimbuko lake kutoka katika moyo wa mwanadamu; amani inayokazia msingi wa haki na mshikamano mintarafu mwanga wa Injili. Amani ni changamoto kubwa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya binadamu kwa siku za usoni.








All the contents on this site are copyrighted ©.