Baba Mtakatifu Francisco, Jumapili akiwahutubia mahujaji na watalii waliokuwa wamekusanyika
katika uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro, kabla ya sala ya Malaika wa Bwana,
alisema, upendo wa Mungu umegubikwa ndani ya upendo kwa jirani. Katika hotuba yake
Baba Mtakatifu, alitoa tafakari fupi juu ya somo la Injili ya siku, ambayo ilikuwa
kutoka Injili Mtakatifu Mathayo 22: 34-40.
Papa alisema, “Injili ya leo
inatukumbusha kwamba sheria zote za Mungu hutuongoza kumpenda Mungu na jirani," na
kwamba "Huwezi kumpenda Mungu bila kumpenda jirani yetu na huwezi kumpenda jirani
bila kumpenda Mungu. Papa aliendelea kusema kwamba, mafundisho mapya ya Kristo yamo
katika muungano wa amri hizi mbili. Aidha aliangalisha katika tafakari ya mtangulizi
wake, Papa Mstaafu Benedict XVI, katika barua yake ya kwanza ya Kitume, Mungu ni
Upendo ” Deus Caritas est,” kipengere namba 16-18 .
Papa Francisco aliendelea
kusema, "Yesu anakamilisha sheria ya agano, kwa umwilisho wake ambamo inamwunganisha
yeye mwenyewe, katika mwili wake, umungu wake na ubinadamu wake , katika siri moja
ya upendo. Na katika mwanga wa neno la Yesu, upendo unakuwa kipimo cha imani, na
imani ni roho ya upendo, na hivyo hatuwezi kutenganisha maisha ya kidini - maisha
ya ucha Mungu , na huduma kwa wake kwa waume, kwa ndugu zetu, wenye mwili na damu
kama sisi tunaokutana nao.
Baada ya sala ya Malaika wa Bwana, Papa Francisco
alilikumbuka tukio la kutajwa kuwa Mwenye Heri, Mama Asunta Marchetti, katika Ibada
iliyofanyika Jumamosi 25 Oktoba, huko Sao Paulo, Brazil . Mama Assunta Marchetti:
mzaliwa wa Italia, ni mwanzilishi wa Shirika la Masista Wamisionari wa Mtakatifu
Charles Borromeo, wanaojulikana kama” The Scalabrinians. Alianzisha shirika hilo
mwishoni mwa karne ya 19 baada ya Askofu wa Piacenza, Giuseppe Scalabrini, ambaye
alisaidia kuanzishwa kwa shirika katika lengo la kudumisha mafundisho ya imani Katoliki
na maisha Katoliki miongoni mwa wahamiaji waliokuwa wakiingia katika nchi zilizojulikana
kwa wakati ule Dunia Mpya. Mpaka sasa utume wa shirika hilo hulenga zaidi kwa wahamiaji,
wakimbizi na watu waliokimbia makazi yao.
Papa Francisco aliendelea kumtaja
Mama Assunta Marchetti kwamba aliiona sura ya Yesu katika watu maskini, yatima,
katika wagonjwa, katika wahamiaji. Na hivyo ni jambo la kumshukuru Bwana kwa uwepo
wa Mama huyo, ambaye anaendelea kuwa mfano wa roho ya Kimisionari na roho ya kujituma
kwa ujasiri bila kuchoka katika huduma ya upendo. Mtumishi huyu wa Mungu anakuwa
uthibitisho wa ukweli kwamba, tunaweza na lazima kuutafuta uso wa Mungu kwa watu
wote wake kwa waume.
Papa Francis pia alitoa salaam zake kwa mahujaji kutoka
pande zote za dunia, na kukitaja rasmi kikundi cha Schoenstatt, ambao siku ya Jumamosi
kilikuwa na mkutano wake hapa Roma, na pia aliikumbuka jamii Peru ambayo ilifika
katika uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro kusali sala ya Malaika wa Bwana, kwa
kufanya maandamano wakiwa wamebeba Sanamu ya Kristo Msulubiwa ya “ El Senor de los
Milagros” - Bwana wa Miujiza – ambayo ilitengenezwa na mtu aliyewekwa huru karne ya
17 huko Lima. Sanamu hiyo sasa inaheshimiwa sana na watu wa Peru kama kielelezo cha
upendo wa kina wa mtu k uyatoa maisha yake kwa ajili ya mwingine na hasa miongoni
mwa watu wa Peru.