2014-10-27 14:10:41

Rais Yoweri Museveni wa Uganda akutana na Papa Francisko mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 27 Oktoba 2014 amekutana na kuzungumza na Rais Yoweri Kaguta Museveni wa Uganda pamoja na msafara wake, uliomtembelea mjini Vatican. Baadaye, Rais Museveni amefanya mazungumzo na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekua ameambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican

Baba Mtakatifu na Rais Museveni wamejadili kwa kina na mapana hali ya maisha ya wanachi wa Uganda pamoja na kuonesha uhusiano mwema uliopo kati ya Serikali ya Uganda, Vatican na Kanisa kwa ujumla, hasa kwa Kanisa kuchangia kwa kiasi kikubwa katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu ya watu. Viongozi hawa wamekazia umuhimu wa watu kuheshimiana na kuthaminiana huku wakiishi kwa amani na utulivu.

Mwishoni, Baba Mtakatifu na Rais Museveni wamegusia pia masuala ya kimataifa, lakini kwa namna ya pekee, maeneo ya Bara la Afrika ambayo kwa sasa yanakabiliana na vita pamoja na kinzani za kijamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.