2014-10-24 14:44:16

Utakatifu ni mwaliko kwa wote!


Wakristo wanaalikwa kwa namna ya pekee kabisa kuchuchumilia utakatifu wa maisha kwani huu ni mwaliko na wito kwa wote na wala si kwa kundi la watu wachache ndani ya Kanisa. Changamoto hii imetiliwa mkazo kwa namna ya pekee kabisa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, ili kuwawezesha Wakristo kuwa kweli ni chumvi ya dunia na mwanga wa mataifa. Lengo ni kuyatakatifuza malimwengu. RealAudioMP3

Mtakatifu Paulo Mtume anapoawaandikia Wakorintho: 1 Kor. 1: 1-2 anawakumbusha kwamba wao wametakatifuzwa kwa njia ya Yesu Kristo, katika: maji na Roho Mtakatifu. Kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo, Wakristo wanafanyika kuwa ni sehemu ya Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa, wakiwa na haki na wajibu unaoambatana na wito huu. Kwa njia ya Ubatizo, Wakristo wanauvua utu wa kale uliochakaa kwa njia ya dhambi na kuanza kujivika utu mpya na kutembea katika mwanga wa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu.

Mtume Paulo katika nyaraka zake anatumia neno “Mtakatifu” kuwaelezea wale waliozaliwa kwa maji na Roho Mtakatifu, yaani, wafuasi wa Kristo. Kumbe, Sakramenti ya Ubatizo inawapatia waamini neema ya utakaso kwa kuwaondolea ile dhambi ya asili. Ni wajibu na jukumu lao kuendelea kuitunza neema ya utakaso waliyoipokea kwa njia ya maisha adili yanayorutubishwa kwa njia ya: Sala, Neno la Mungu, Sakramenti za Kanisa na matendo ya huruma, kielelezo makini cha imani katika matendo.

Kwa njia ya Ubatizo, Wakristo wametengwa na dhambi na hivyo kuunganishwa na Kristo ambaye ni: njia, ukweli na uzima. Kumbe, Wakristo wanapaswa kuchangamkia utakatifu wa maisha kama sehemu ya mchakato endelevu wa maisha yao. Hii ni safari ndefu inayojikita katika uhalisia wa maisha ya kila siku na kwamba, kila mwamini akitaka na kuinua anaweza kuwa mtakatifu kwani huu ni mwaliko na wito kwa wote, jaribu, utagundua siri ya mafanikio.

Na Padre Richard Mjigwa, C.PP. S.,
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.