Upendo na ukweli vivunjilie mbali vizingiti vinavyokwamisha umoja wa Kanisa
Wanachama wa Mfuko wa "Orientale Lumen" unaosimamiwa na Askofu mkuu Kallistos wa Jimbo
kuu la Diokleia wanaendelea na hija ya maisha ya kiroho mjini Roma kama sehemu ya
mchakato wa kutaka kufanya maboresho katika maisha yao ya kiroho, kwa kushikamana
zaidi na Yesu, chimbuko la imani na mlango wa utimilifu wao. Ni hija inayojielekeza
katika mchakato wa upatanisho, ili kujenga na kuimarisha umoja kamili kati ya Wakristo.
Baba
Mtakatifu Francisko akizungumza na wajumbe hawa siku ya Ijumaa tarehe 24 Oktoba 2014
mjini Vatican amekumbusha kwamba, hakuna majadiliano ya kweli ya kiekumene yasiyojikita
katika dhamana ya mabadiliko ya ndani sanjari na kuhakikisha kwamba, waamini wanakuwa
waaminifu kwa Kristo pamoja na kutekeleza mapenzi yake.
Baba Mtakatifu amewapongeza
wajumbe hawa kwa hija hii ambayo pamoja na mambo mengine inapenda kuwakumbuka kwa
namna ya pekee Watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II, waliotangazwa na Mama Kanisa,
Aprili, 2013; viongozi waliojielekeza zaidi katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene
na Makanisa ya Kiorthodox kutoka Mashariki. Ni viongozi ambao wameonesha ari na moyo
wa kutaka kukuza na kudumisha umoja miongoni mwa Wakristo, ili wote waweze kuwa wamoja
chini ya Kristo.
Mtakatifu Yohane XXIII alipokuwa anatangaza nia yake ya kuitisha
Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, alipania kuona umoja miongoni mwa Wakristo, dhamana
iliyoendelezwa kwa ari kubwa na Mtakatifu Yohane Paulo II katika maisha na utume wake
kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, kama inavyojidhihirisha katika Waraka wake wa Kichungaji,
Ut Unum Sint, "Ili Wote Wawe Wamoja".
Baba Mtakatifu amewaomba wajumbe hao
wakati wa hija yao ya kitume mjini Roma kumkumbuka katika sala zao, ili aweze kutekeleza
dhamana na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, kwa ajili ya huduma ya mshikamano
na umoja ndani ya Kanisa kwa kufuata mapenzi ya Kristo mwenyewe.
Baba Mtakatifu
Francisko amewataka pia kumfikishia salam na matashi mema Patriaki Bartolomeo wa kwanza
watakapomtembelea na kukumbusha kwamba, hata Yeye mwenyewe amekubali mwaliko na kwa
sasa anajiandaa kwenda kumtembelea ili kwa pamoja waweze kuadhimisha Siku kuu ya Mtakatifu
Andrea, kama kielelezo makini cha umoja na mshikamano kati ya Roma na Costantinopoli,
ili kuvunjilia mbali kwa njia ya upendo na ukweli vizingiti ambavyo vinakwamisha umoja
wa Kanisa.