2014-10-23 14:21:47

Waziri mkuu wa Grenada akutana na Papa mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko mapema siku ya Alhamisi asubuhi, tarehe 23 Oktoba 2014 alikutana na kuzungumza na Waziri mkuu wa Grenada Bwana Keith Mitchel ambaye baadaye alikutana pia na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambatana na Askofu mkuu Dominic Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Katika mazungumzo baina ya viongozi hawa wawili, kwa pamoja wameridhishwa na mahusiano bora yaliyopo kati ya pande hizi pamoja na kusifia mchango wa Kanisa Katoliki nchini Grenada katika sekta ya elimu, afya na huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Vijana ni kati ya changamoto kubwa inayoikabili Serikali ya Grenada.

Baba Mtakatifu na mgeni wake wameonesha umuhimu wa wadau mbali mbali nchini Grenada kuendelea kushirikiana kwa karibu zaidi katika mchakato unaopania kukoleza maendeleo ya watu: kiroho na kimwili pamoja na mafao ya wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.