Waziri mkuu wa Grenada akutana na Papa mjini Vatican
Baba Mtakatifu Francisko mapema siku ya Alhamisi asubuhi, tarehe 23 Oktoba 2014 alikutana
na kuzungumza na Waziri mkuu wa Grenada Bwana Keith Mitchel ambaye baadaye alikutana
pia na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambatana na Askofu
mkuu Dominic Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa
mjini Vatican.
Katika mazungumzo baina ya viongozi hawa wawili, kwa pamoja
wameridhishwa na mahusiano bora yaliyopo kati ya pande hizi pamoja na kusifia mchango
wa Kanisa Katoliki nchini Grenada katika sekta ya elimu, afya na huduma kwa maskini
na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Vijana ni kati ya changamoto kubwa inayoikabili
Serikali ya Grenada.
Baba Mtakatifu na mgeni wake wameonesha umuhimu wa wadau
mbali mbali nchini Grenada kuendelea kushirikiana kwa karibu zaidi katika mchakato
unaopania kukoleza maendeleo ya watu: kiroho na kimwili pamoja na mafao ya wengi.