Watu wanateseka kutokana na athari za ugonjwa wa Ebola!
Askofu Anthony Falla Borwah wa Jimbo Katoliki la Gbarnga, Liberia, amewataka waamini
na watu wote wenye mapenzi mema kuonesha mshikamano wa dhati na wananchi wa Liberia
ambao wamekumbwa na ugonjwa wa Ebola, ili waweze kupata matumaini na kusonga mbele
licha ya mateso na changamoto wanazokabiliana nazo kutokana na madhara ya ugonjwa
wa Ebola. Anasema kuna watu wanaoendelea kupoteza maisha yao kutokana na magonjwa
na njaa lakini kuna kundi kubwa la watu ambao wamekata tamaa ya maisha.
Askofu
Borwah anaiomba Jumuiya ya Kimataifa kujifunga kibwebwe ili kuwasaidia watu walioathirika
kutokana na maambukizi ya ugonjwa wa Ebola huko Afrika Magharibi. Watu wanakabiliwa
na baa la njaa na kwamba, shughuli za kiuchumi na kijamii zinaendelea kudorora kutokana
na hofu ya maambukizi ya ugonjwa wa Ebola, ambao kwa sasa umekuwa ni tishio kubwa
kwa Jumuiya ya Kimataifa. Kutokana na hofu ya ugonjwa wa Ebola, utu na heshima ya
binadamu vinaanza kuwekwa rehani; watu wanashindwa kufarijiana kutokana na majonzi
makubwa yanayowasibu kwa wakati huu.
Askofu Borwah anaiomba Jumuiya ya Kimataifa
kuendelea kufanya utafiti wa kina ili kubainisha chanzo cha ugonjwa wa Ebola na jinsi
ambavyo watu wanaweza kupata kinga na hatimaye tiba, ili watu waweze kutambua na kuonja
tena umuhimu wa zawadi ya maisha. Kanisa linaendelea kuchangia kwa hali na mali katika
mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ebola, kwa kujiwekea mikakati ya muda mrefu na mfupi
kwa siku za usoni.