2014-10-22 08:17:49

Huduma makini kwa watoto wagonjwa ni kielelezo cha upendo wa Kanisa kwa watoto!


Hospitali ya Bambino Gesù inayomilikiwa na kuendeshwa na Vatican, Jumanne tarehe 21 Oktoba, 2014 imezindua maabara mpya ambazo zitatumika kwa ajili ya kufanya tafiti na uchunguzi kwa magonjwa ya watoto kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Ni maabara ambayo ni ya kisasa katika kukabiliana na magonjwa tete yanayowasumbua watoto.

Tukio hili limehudhuriwa na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican ambaye pia ni Rais wa Hospitali ya Bambino Gesù. Maabara hizi zitaweza kutumika na watafiti 150 na kwamba, hadi kukamilika kwake zimegharimu jumla ya Euro millioni 26.

Kardinali Parolin amewashukuru viongozi na wafanyakazi wa Hospitali ya Bambino Gesù katika jitihada zaao zinazopania kutoa huduma bora na makini kwa watoto wadogo kutoka sehemu mbali mbali za dunia, kwa kuwa na tafiti makini zinazotumia vyombo vya kisasa zaidi. Kuna magonjwa ambayo yanaendelea kuwasumbua watoto, kumbe Hospitali ya Bambino Gesù haina budi kuhakikisha kwamba, inakuwa na vifaa tiba vitakavyotumika kuwahudumia watoto wagonjwa na Jamii katika ujumla wake.

Kardinali Parolin anasema, ustaarabu wa jamii yoyote ile unapimwa kwa kuangilia jinsi ambavyo jamii husika inawajali na kuwahudumia: wagonjwa, maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Kanisa limeendelea kuwa mstari wa mbele katika utoaji wa huduma za kijamii, kama kielelezo cha mshikamano na maskini pamoja na wote wanaohitaji kuonjeshwa huruma na upendo wa Mungu, kielelezo makini cha imani tendaji, hasa kwa njia ya huduma kwa watoto wagonjwa.

Tangu kuanzishwa kwa Hospitali ya Bambino Gesù, Mababa Watakatifu wamechangia kwa namna ya pekee katika kuendeleza huduma zinazotolewa na Hospitali ya Bambino Gesù kama sehemu ya mikakati yao ya shughuli za kichungaji kwa watoto wagonjwa. Hospitali hii ni kielelezo makini cha huduma ya upendo inayotolewa na Baba Mtakatifu, changamoto kwa wafanyakazi kuendelea kuwa ni mfano wa kuigwa katika taaluma, ukweli na uwazi; ukarimu unaozingatia tunu msingi za kiutu na Kikristo pamoja na kujenga mazingira ambamo kila mtu anajisikia kuwa ni mdau katika kulinda, kutetea na kuendeleza Injili ya uhai, hata pale sadaka kubwa zaidi inapohitajika.

Hospitali ya Bambino Gesù haina budi kuendelea kuwa ni kielelezo cha huduma makini kwa watoto wagonjwa pamoja na familia zao wanaojikabidhi kwa Mtoto Yesu ili kupata tiba ya magonjwa yanayowasumbua. Anawatakia wadau wote huduma makini pamoja na kujali mahangaiko ya wazazi wanaowahudumia watoto wao Hospitalini hapo.







All the contents on this site are copyrighted ©.