2014-10-21 08:08:30

Wahamasisheni watu kumkubali, kumpenda na kumwongokea Kristo kwa njia ya ushuhuda wa maisha yenu!


Maadhimisho ya Siku ya 88 ya Kimissionari Duniani kwa Mwaka 2014 yamepambwa kwa namna ya pekee na Baba Mtakatifu Francisko kumtangaza Papa Paulo VI kuwa Mwenyeheri, kiongozi ambaye alijitaabisha kuhakikisha kwamba, Habari Njema ya Wokovu inawafikia watu wa mataifa. RealAudioMP3

Ilikuwa ni siku ya kufunga rasmi maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu familia, tayari kuendeleza mchakato wa Mama Kanisa katika azma yake ya kutangaza Injili ya Familia kadiri ya mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu.

Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican anawakumbusha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kwamba, Yesu Kristo ni njia, ukweli na uzima. Ndiye binadamu aliyekamilika kwani ni Mwana mpendwa wa Mungu, Nafsi ya Pili katika Fumbo la Utatu Mtakatifu. Siku ya Kimissionari Duniani inalenga kuwahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema wakubali, wapende na wafurahie kumpokea Yesu Kristo kwa moyo wa toba na wongofu wa ndani.

Ni mwaliko na changamoto ya kuachana na dhambi pamoja na mambo yote yanayosigana na mpango wa Mungu katika hija ya maisha ya binadamu. Kimsingi watu wanahamasishwa kuachana na dhambi na mambo yote yanamkanganya mwanadamu katika ulimwengu mamboleo, ili kumpatia nafasi Yesu Kristo aweze kuwakirimia neema na baraka katika hija ya maisha yao kwa njia ya Kanisa.

Wakristo watambue kwamba, kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo wanatumwa kutangaza Injili hadi miisho ya dunia kwa njia ya ushuhuda amini wa maisha yao yanayopata chimbuko lake kwa kukutana na kutembea pamoja na Yesu katika maisha yao ya kila siku. Wakristo wasaidie kuwafundisha watu kuyashika mafundisho ya Kristo, ili kweli Injili iweze kupenya na kuleta upya wa maisha, ili kuweza kumkamilisha mwanadamu katika hija ya maisha yake hapa duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.