2014-10-21 15:05:40

Papa Francisko kutembelea Uturuki, tarehe 28 - 30 Novemba 2014


Baba Mtakatifu Francisko anatarajia kufanya hija ya kichungaji nchini Uturuki kuanzia tarehe 28 hadi tarehe 30 Novemba 2014, kufuatia mwaliko kutoka kwa Rais wa Uturuki, Patriaki Bartolomeo wa kwanza na Baraza la Maaskofu Katoliki Uturuki. Akiwa nchini humo atatembelea miji ya Ankara na Istanbul.

Baba Mtakatifu anatarajiwa kuondoka mjini Vatican, Ijumaa tarehe 28 Novemba 2014 na kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Esemboga, ulioko mjini Ankara majira ya saa 7:00 mchana na hapo atapokelewa rasmi na atimaye kutembelea Makumbusho ya Ataturk. Atakaribishwa rasmi na baadaye atafanya mazungumzo ya faragha na Rais kwenye Ikulu pamoja na kuzungumza na viongozi wa Serikali. Baadaye, Baba Mtakatifu atamtembelea Waziri mkuu wa Uturuki pamoja na Waziri wa masuala ya kidini nchini humo.

Jumamosi tarehe 29 Novemba 2014 majira ya saa 3:30 asubuhi, Baba Mtakatifu ataondoka kutoka mjini Ankara kuelekea Istanbul anakotarajiwa kuwasili saa 4:30. Hapo atatembelea Jumba la Makumbusho la Sofia, Msikiti mkuu wa Sultan Ahmet pamoja na kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Roho Mtakatifu. Baba Mtakatifu baadaye atahudhuria Ibada ya Kiekumene kwenye Kanisa la Kipatriaki la Mtakatifu George na baadaye kukutana kwa faragha na Patriaki Bartolomeo wa kwanza.

Jumapili tarehe 30 Novemba 2014, Baba Mtakatifu Francisko pamoja na ujumbe wake, wataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu peke yao na baadaye kufuatia Liturujia ya Neno itakayoadhimishwa kwenye Kanisa kuu la Kipatriaki la Mtakatifu George. Hapa viongozi hawa wawili watatoa baraka ya kiekumene pamoja na kutia sahihi tamko la pamoja. Baba Mtakatifu amealikwa kwa chakula cha mchana na Patriaki Bartolomeo wa kwanza, hapa Baba Mtakatifu anatarajiwa kutoa hotuba ya shukrani na baadaye jioni kuondoka kurudi mjini Vatican







All the contents on this site are copyrighted ©.