Jubilee ya Miaka 200 tangu kuanzishwa kwa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya
Yesu ulimwenguni! Dodoma kuwaka moto hapo mwaka 2015
Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu kila mwaka ifikapo tarehe 21 Oktoba
linaadhimisha Siku kuu ya Mwalilishi wa Shirika lao, Mtakatifu Gaspar del Bufalo,
Mtume hodari wa Damu Azizi ya Yesu. Kwa kipindi cha miaka mitatu, Wamissionari hawa
wanaendelea na maandalizi ya maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 200 tangu Mtakatifu Gaspar
alipoanzisha Shirika hili ambalo kwa sasa limeenea sehemu mbali mbali za dunia.
Shirika la
Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti ya Tanzania hapo tarehe 15 Agosti 2015
litakuwa ni Kanda kamili inayojitegemea kwa maisha na utume wake. Kwa sasa Vikarieti
ya Tanzania iko chini ya Kanda ya Italia. Padre Eugen Nchimbi atashirikisha zaidi
matendo ya Mungu katika maisha yao!
Tarehe 21 Mwezi Oktoba kila mwaka, Wamisionari
wa Damu Azizi ya Yesu (yaani C.PP.S) duniani kote tunaadhimisha Sherehe ya Mtakatifu
Mwanzilishi wa Shirika letu, Gaspari Del Bufalo. Katika uhai wake (1786-1837), Gaspari
Del Bufalo, kupitia yafuatayo:
malezi ya wazazi wake (Antonio na
Annunciata); kupitia mang’amuzi ya kupona (toka hatari ya kupofuka macho)- kwa
maombezi ya mama yake kwa Mt. Fransisko Ksaveri; machafuko ya kisiasa na uchumi
ya wakati wake yaliyoikumba Roma na Italia kwa ujumla, ikiwemo umaskini wa watu, uvamizi
wa Napoleoni Bonapart, ugumu wa maisha ya gerezani (1810-1814) na kushuka kwa imani
na maadili, kulipuka kwa ugonjwa wa kipindupindu.
Aling’amua kuwa
Mungu anawapenda watu wote na ili kuwakomboa alimtoa Mwanaye wa pekee, Yesu Kristo
aliyemwaga Damu yake azizi pale Msalabani na anawaalika watu wote kuutambua upendo
huo, kugeuza mwenendo wa maisha- kujipatanisha na Mungu; kisha kuwa wajumbe wa upendo
huo wa Mungu, kiasi cha kuwafariji wote walio katika mahangaiko ya kimwili na kiroho.
Kwa
kuzingatia ucha-Mungu uliodhihirika katika ibada yake kwa Damu ya Ukombozi, mahubiri
ya hadharani, ushupavu wake kupitia huduma kwa maskini, huduma kwa wagonjwa na jitihada
ya kuwaongoa majambazi; kifo chake cha Desemba 28, 1837 kilifuatiwa na kutambulika
kwake, yaani: mwaka 1904 Papa Pio X alimtangaza kuwa Mwenye heri na tarehe 12 Mwezi
Juni 1954 alitangazwa na Papa Pio XII kuwa Mtakatifu. Licha ya Papa Pio XII, Mapapa
wengine kama vile: Yohane XXIII, Yohane Paulo II, walimtambua kuwa Mtume wa Damu Azizi.
Shirika
la Wamisionari wa Damu Azizi ya Yesu (CPPS) lililoanzishwa na Gaspari Del Bufalo hapo
tarehe 15 Agosti 1815 huko Abasia ya Mt. Felix, kijijini Giano, mkoani Umbria nchini
Italia, kwa neema ya Mungu limefanikiwa kusambaa kote duniani, limejaliwa wamisionari
na wafuasi wengi na mwakani, yaani 2015, litatimiza miaka 200 tangu kuanzishwa kwake.
Ili
kujiandaa kuadhimisha vemaJjubilee hiyo, kumefanyika maandalizi ya miaka mitatu ya
maandalizi kila mwaka ukiwa na mada ya kutakakari; yaani: 2012/2013: Historia ya Mwanzilishi
na ya Shirika; 2013/2014 Karama ya upatanisho na hatimaye, 2014/2015 jitihada za kujibu
kwa vitendo kilio cha Damu (mahangaiko ya watu duniani).
Na katika mwaka wenyewe
wa Jubilei yaani 2015, matukio mawili yatafanyika nchini Italia yakihudhuriwa na Familia
ya Damu Azizi toka duniani kote:
Kongamano la Vijana tarehe 3-6
Januari huko Fraskati (vijana wanaalikwa kujiandikisha kuhudhuria)- mada ya kongamano
ni maneno ya Mt. Gaspari Del Bufalo “natamani kuwa na lugha elfu” – ili kufikisha
kwa watu wote upendo wa Mungu aliyetukomboa kwa kumwaga Damu yake azizi. Hija na
maadhimisho ya Kilele tarehe 29 Juni hadi tarehe 5 Julai 2015 huko Roma, Italia (watu
wote wanaalikwa kujiandikisha kwa Wamisionari wa Damu Azizi nchini Tanzania.
Sanjari
na maadhimisho hayo ya kidunia, Wakuu mbalimbali wa Shirika la Wamisionari wa Damu
Azizi, katika mkutano wao uliofanyika tarehe 13-22 Septemba 2014 huko Dodoma, Tanzania,
waliridhia ombi la Vikarieti ya Tanzania kupandishwa hadhi toka Vikarieti kuwa Kanda
kamili inayojitegemea. Sherehe ya kuzaliwa kwa Kandai hiyo mpya itaadhimishwa katika
kilele cha Jubilei ya miaka 200 tangu kuanzishwa Shirika, yaani, tarehe 15 Agosti
2015 huko mjini Dodoma, Tanzania.
Hivyo ndivyo ilivyo kwa Wamisionari wa Damu
Azizi ya Yesu Vikarieti ya Tanzania, wakisukumwa na moyo wa umisionari katika kueneza
upendo kwa Damu Azizi ya Yesu wakiongozwa na kauli mbiu “ndoto ya Mtakatifu Gaspari
inaendelea”, wanawaalika watu wote kusali na kushiriki kwa dhati ili Jubilei hii ituunde
upya, vizuri na kwa namna endelevu.
Lengo hilo, linawezakana kwa njia ya Damu
ya thamani kubwa ya Bwana wetu Yesu Kristo iliyomwagika kwa ajili ya wokovu wa wengi.
Isifiwe na kuabudiwa Damu Azizi ya Kristo, Milele Amina.