2014-10-20 12:25:35

Msishabikie mambo yanayosigana na mpango wa Mungu katika kazi ya uumbaji!


Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania amewataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwa waaminifu kwa mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu kwa kujikita katika kanuni maadili, huku wakiheshimu maumbile na kuachana na upuuzi wa walimwengu wanaotaka kushabikia vitendo vya ushoga! RealAudioMP3

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Askofu Ngalalekumtwa anabainisha kwamba, Mababa wa Sinodi wakati wa maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kuhusu familia wametafakari kwa kina na mapana baraka ambayo Mwenyezi Mungu amemkirimia mwanadamu kwa kumshirikisha katika kazi ay uumbaji, inayofanywa ndani ya familia inayoundwa na Bwana na Bibi, ili waweze kukamilishana na kutakatifuzana katika hija yao ya maisha.

Askofu Ngalalekumtwa anasema ni mpango wa Mungu kwamba, binadamu aweze kuzaliwa na kupata malezi na makuzi kutoka ndani ya familia, ili watoto nao waweze kujifunza matendo makuu ya Mungu kwa njia ya Baba na Mama zao wanaowakirimia mazingira bora ya malezi na makuzi.

Ushoga ni mambo yanayosigana na mpango wa Mungu katika kazi ya uumbaji na malezi kwa watoto. Kanisa linatambua ndoa kuwa Sakramenti inayoonesha upendo wa Kristo kwa Kanisa lake, changamoto kwa binadamu kujikita katika kanuni maadili, utu wema, nidhamu pamoja na kuheshimu maumbile na kamwe wasipende kushabikia mambo yanayosigana na mpango wa Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.