2014-10-18 09:49:44

Baa la njaa linatishia amani na usalama duniani!


Baba Mtakatifu Francisko katika maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani hapo tarehe 16 Oktoba 2014 amemwandikia ujumbe Bwana Josè Graziano da Silva, Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa, FAO, akionesha ni kwa jinsi gani ambavyo baa la njaa linavyotishia amani na usalama wa Jumuiya ya Kimataifa na hivyo kuitaka Jumuiya ya Kimataifa kuibua mbinu mkakati makini utakaozisaidia Jamii za wakulima vijijini kuzalisha chakula cha kutosha pamoja na kupambana na umaskini.

Baba Mtakatifu katika ujumbe huo anapenda kuwa ni sauti ya watu wanaoteseka kutokana na baa la njaa wakati kuna chakula kingi duniani, kinachotupwa kwenye mashimo na mapipa ya taka, kutokana na ubinafsi unaowasukuma baadhi ya watu kupenda kupata faida kubwa zaidi.

Baa la njaa ni kati ya majanga makubwa yanayomwandama mwanadamu, lakini ni janga ambalo bado linaangaliwa kwa "jicho la kengeza" bila kuvaliwa njuga, licha ya maendeleo makubwa yaliyokwisha kupatikana katika nchi mbali mbali. Serikali nyingi zimeondoa ruzuku kwa masuala ya kijamii, hali ambayo inaendelea kugumisha maisha ya watu wengi duniani. Kuna kundi kubwa la watu linalo kabiliwa na baa la njaa na utapiamlo, ikumbukwe kwamba, hapa binadamu anapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza na wala si namba.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, haitoshi kutoa msaada kama mbinu ya kupambana na baa la njaa bali kubadilisha sera na mikakati ya maendeleo, ili kuharakisha mchakato wa maendeleo kwa kurekebisha sheria na kanuni za Jumuiya ya Kimataifa, ili kujenga na kuimarisha amani ambayo kwa sasa iko mashakani kutokana na baa la njaa.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Mkurugenzi mkuu wa FAO anabainisha kwamba, kauli mbiu iliyokuwa imechaguliwa kwa ajili ya maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani kwa Mwaka 2014: "Familia za Wakulima, Lisheni dunia na tunzeni mazingira" inaonesha umuhimu wa familia za wakulima vijijini zinavyoweza kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya baa la njaa ikiwa kama zitawezeshwa kikamilifu, kwani wao wanaweza kuchangia uhakika wa usalama wa chakula duniani pasi na kuharibu mazingira.

Baba Mtakatifu anasema, ili kufikia lengo hili, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa mahitaji ya mtu mzima: kiroho, kimwili na kijamii na wala si kwa kuangalia teknolojia peke yake; sanjari na kujenga mshikamano wa upendo na udugu, unaowawezesha watu kushirikiana na kusaidiana katika kuendeleza gurudumu la maisha ya kijamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.