Ujumbe wa Baba Mtakatifu kwa Siku ya 88 ya Kimissionari Duniani kwa Mwaka 2014
Mama Kanisa tarehe 19 Oktoba 2014 anaadhimisha Siku ya 88 ya Kimissionari Duniani,
iliyoanzishwa kunako mwaka 1926 na Papa Pio wa Kumi na moja na kuanza kuadhimishwa
rasmi hapo mwaka 1927 kama siku ya kukoleza ari moyo wa kimissionari katika kuwatangazia
Watu wa Mataifa Habari Njema ya Wokovu. Hii ni siku ambayo inaadhimishwa mwezi Oktoba,
ambao kimsingi ni mwezi wa kimissionari.
Baba Mtakatifu
Francisko katika ujumbe wake kwa maadhimisho ya Siku ya 88 ya Kimissionari Duniani
kwa mwaka 2014 anasema kuna umati mkubwa wa watu ambao haujabahatika kusikia Habari
Njema ya Wokovu, Familia yote ya Mungu inawajibika kushiriki katika Uinjilishaji kwa
kutambua kwamba, Kanisa limeanzishwa na linatumwa kuwatangazia watu juu ya Ufalme
wa Mungu.
Hii ni siku ambayo waamini wanaalikwa kushiriki kikamilifu kwa njia
ya sala na sadaka yao ili kuonesha mshikamano na Makanisa machanga duniani kama njia
ya kumshukuru Mungu kwa neema sanjari na kuonesha ile furaha ya ndani. Yesu anawatuma
wafuasi wake na kuwategemeza katika shughuli za kimissionari kama inavyojionesha katika
Maandiko Matakatifu pale alipowatuma wafuasi wake Sabini na wawili, wakarudi huku
wakiwa wamesheheni furaha baada ya kutangaza kuhusu Ufalme wa Mungu na kuwaandaa watu
kukutana na Yesu.
Mitume wanapoonesha furaha yao, Yesu anawataka wafurahi
kwa sababu majina yao yameandikwa mbinguni na kwamba, wamebahatika kuyaona matendo
makuu ya Mungu yakitendwa mbele ya macho yao! Hii si nguvu ya kutoa pepo wachafu,
bali ile nguvu ya upendo ambao wamekirimiwa na Mwenyezi Mungu. Uzoefu na mang'amuzi
haya yanakuwa ni sababu ya furaha hata kwa Yesu Mwenyewe kiasi cha kumshukuru Roho
Mtakatifu, huku akimtolea sifa Baba yake wa mbinguni, kwani ile siri kubwa kuhusu
Ufalme wa Mungu iliyokuwa imefichika inajionesha kwa njia ya Yesu Kristo na ushindi
wake dhidi ya shetani.
Hii ni siri ambaye imefunuliwa kwa maskini na wanyenyekevu
wa moyo ambao wamebarikiwa mbele ya Mungu. Hawa ni kama Bikira Maria na Mtakatifu
Yosefu, Wavuvi kutoka Galilaya na Mitume wote ambao wamebahatika kushikamana na Yesu
wakati alipokuwa anawahubiria watu Habari Njema ya Wokovu.
Baba Mtakatifu anasema,
Yesu anaonesha ile furaha inayobubujika kutoka katika undani wake kutokana na ufunuo
wa mpango wa Mungu katika kazi ya ukombozi wa mwanadamu, kielelezo cha hali ya juu
kabisa cha upendo wa Mungu kwa mwanadamu kwa njia ya Yesu Kristo. Hii ndiyo furaha
iliyokuwa inabubujika kutoka moyoni mwa Bikira Maria pale alipomtembelea binamu yake
Elizabeti kumshirikisha kuhusu matendo makuu ya Mungu katika maisha yake.
Hii
ndiyo furaha inayoendelea kububujika katika maisha ya waamini hadi nyakati hizi, anasema
Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa maadhimisho ya Siku ya themanini na
nane ya Kimissionari Duniani na kuwawezesha waamini kuingia katika maisha ya Fumbo
la Utatu Mtakatifu. Mungu Baba ni chemchemi ya furaha, Yesu Kristo ni kielelezo cha
furaha hii na Roho Mtakatifu ndiye mwezeshaji mkuu, changamoto kwa waamini kumjifunza
na kumwendea Yesu ili aweze kuwafariji na kuwakirimia maisha ya uzima wa milele, wale
wote wanaobahatika kukutana na Yesu.
Wale wanaokombolewa na Yesu, wanaondolewa
dhambi, hofu na "jangwa la maisha ya kiroho" kwani kwa njia ya Yesu, daima waamini
wanaweza kupata na kuendelea kububujika furaha. Hivi ndivyo ilivyokuwa kwa Bikira
Maria pamoja na Mitume wake walioamua kubaki pamoja na Yesu ili kushiriki azma ya
Uinjilishaji, Yesu akawa ni sababu ya furaha yao ya ndani!
Baba Mtakatifu Francisko
anasema ulimwengu mamboleo unakabiliwa na hatari kubwa ya kumezwa na ulaji wa kupindukia
unaojikita katika ubinafsi, mambo yanayousononesha moyo wa binadamu kwa kutaka furaha
za mpito pamoja na dhamiri mfu. Binadamu anachangamotishwa kujichotea wokovu ulioletwa
na Yesu, wafuasi wake wakiwa wa kwanza kuguswa na upendo wake ili kuwa kweli ni vyombo
vya Injili ya Furaha, ili kushiriki ile furaha ya uinjilishaji.
Maaskofu wana
dhamana ya kwanza kabisa katika utekelezaji wa mchakato wa Uinjilishaji, kwa kujenga
na kuimarisha umoja wa Kanisa mahalia na kuendeleza utume wa Kimissionari hadi miisho
ya dunia, hasa katika maeneo yaliyoko pembezoni mwa dunia, huko ambako kuna maskini
wanaosubiri kwa hamu kubwa kusikia Habari Njema ya Wokovu.
Upungufu wa miito
ya Kipadre na Kitawa ni kielelezo cha Jumuiya kukosa ile furaha yenye mvuto na mguso,
inayobubujika kwa mwamini kukutana na Yesu kwa kuwashirikisha pia maskini. Hii ni
changamoto kwa Parokia na Vyama vya Kitume kuonesha ushuhuda wa udugu unaojikita katika
upendo wa Yesu pamoja na kuguswa na shida pamoja na mahangaiko ya maskini na wote
wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Pale ambapo kuna furaha ya kweli, hapo pia kuna
ari na moyo wa kutaka kuwashirikisha wengine, hapo ni mwanzo wa miito mitakatifu.
Waamini walei wanahamasishwa pia kushiriki maisha ya kimissionari, ili kutangaza Injili,
lakini wanahitaji majiundo makini.
Baba Mtakatifu anasema kwamba, Siku ya Kimissionari
Duniani ikuze ndani ya waamini wajibu wa kimaadili wa kushiriki kwa furaha utume wa
kuwatangazia Watu wa Mataifa Habari Njema ya Wokovu, kwa kuchangia kwa hali na mali,
kwa kutambua kwamba, sadaka hii ni sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji wa watu unaobubujika
kutoka katika upendo.
Baba Mtakatifu anawataka waamini katika Makanisa mahalia
kutokubali kupokwa ile furaha ya Uinjilishaji. Anawaalika kujizamisha katika furaha
ya Injili kwa kuirutubisha kwa upendo. Furaha ya mfuasi wa Kristo inajionesha kwa
kukaa na Yesu, mwamini anapotekeleza mapenzi ya Mungu na anaposhirikisha imani, matumaini
na mapendo ya Kiinjili.
Imehaririwa na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.